Somalia : mmoja wa watuhumiwa wakuu wa uharamia awekwa mbaroni
Vyombo vya usalama nchini Somalia vimedai kufanikiwa kumtia mbaroni mmoja wa watuhumiwa wakuu wanaoendesha mtandao wa maharamia wanaoteka meli kwenye pwani ya bahari ya Hindi.
Imechapishwa:
Polisi mjini Mogadishu wamethibitisha kukamatwa kwa Mohamed Garfanji siku ya Jumapili jioni akiwa na walinzi wake wenye silaha ambapo polisi walipokea taarifa toka kwa wananchi kuhusu eneo aliko kiongozi huyo.
Mohamed Garfanji ni miongoni mwa watuhumiwa wakuu wa uharamia ambao wamehusika na matukio ya utekaji meli kubwa za kigeni zinazopita kwenye eneo la pwani ya Somalia na kujipatia mamilioni ya fedha baada ya kulipwa na wamiliki wa meli hizo ili kuziachia.
Mwaka jana rais Hassan Sheikh Mohamud alitangaza kutoa msamaha kwa maharamia wadogo kujisalimisha na kuacha shughuli zao, hatua aliyochukua kujaribu kumaliza uharamia kwenye bahari yake lakini akasema msamaha huo hautawahusu viongozi wao.
Marekani na Sychelles zinataka kumuhoji mtuhumiwa huyo kwa madai ya kuhusika kwenye utekaji wa raia wake.