Burundi: mvutano wa kisiasa waendelea kushuhudiwa
Zoezi la kujiorodhesha kwenye daftari la wapiga kura ambalo linatazamiwa kuanza Jumatatu Novemba 24 nchini Burundi, limezua hisiasa tofauti katika jamii ya wanasiasa nchini humo pamoja na raia wa jijini Bujumbura.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 04:18
Mvutano umeanza kujitokeza kati ya wanasiasa nchini Burundi wakati zikisalia siku nne ili zoezi la kujiorodhesha kwenye daftari la wapiga kura lianze.
Wanasiasa hao wameanza kulaumiana, huku tume huru ya kitaifa ya uchaguzi (Ceni) ikiendelea kunyooshewa kidole cha lawama kwamba haiwajibiki kwa kazi yake.
Upinzani umekua ukiituhumu tume hiyo kuegemea upande wa chama tawala na kuwa kibaraka cha utawala. Upinzani umeomba zoezi hilo liahirishwe.
Kwa upande wake mwenyekiti wa tume huru ya kitaifa ya uchaguzi, Pierre-Claver Ndayicariye, amesema kazi ya Ceni haiwezi kumfurahisha kila mwanasiasa.
" Kunabaadhi wanaoridhishwa na kazi inayotekelezwa na tume hiyo na kuna wengine ambao wataendelea tu kupinga na kuikosoa Ceni" , amesema Pierre-Claver Ndayicariye.
Ndayicariye amewatolea wito raia kuitikia zoezi hilo litakaloanza Jumatatu Novemba 24.