Askari wa Chad wajiondoa katika kambi yao ya Aguelhok, Mali
Askari wa Chad waliotumwa Mali wameghadhibishwa kwa mara nyingine tena. Kwa mujibu wa baadhi ya vyanzo, mamia kadhaa miongoni mwao, wamejiondoa katika kambi yao ya Aguelhok, kaskazini mwa Mali.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Usiku wa Jumanne kuamkia Jumatano Novemba 26, wanajeshi wa kikosi cha Umoja wa Mataifa kutoka Chad, waliondoka kwenye ngome hiyo muhimu katika jimbo la Kidal na kuhamia kwenye umbali wa kilomita zaidi ya mia moja kusini mwa Mali. Wanajeshi hao wanadai marupurupu na mishahara.
Wakiwa katika magari kadhaa, baadhi ya askari wa kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Mali kutoka Chad waliondoka kwenye kambi yao ya Aguelhok katika jimbo la Kidal, na kwa sasa wamepiga kambi katika jimbo la Anefis, kusini mwa Mali. Wanajeshi hao ni zaidi ya mia moja, kulingana na tangazo liliyotolewa na mmoja kati ya askari hao wa Chad ambaye ameongea na RFI.
“ Tunadai marupurupu na mishahara tangu miezi mitatu iliyopita”, ameeleza kwa simu askari huyo.
" Hatutorudi Aguelhok Kama tatizo hili litakua halijapatiwa suluhu, hapo tumemaliza", ameongeza askari huyo.
Kwa upande wake, chanzo cha usalama katika jimbo la Kidal, mbali na madai hayo ya marupurupu na mishahara, huenda kuna mataizo mengine ya ndani katika kikosi hicho kutoka Chad. Hii ni taarifa mbaya kwa kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Mali. Askari wa Chad kuondoka katika kambi yao ya Aguelhok, ni kuwapa fursa wapiganaji wa makundi ya kiislam kuendelea na harakati zao kaskazini mwa Mali.
Mwaka uliyopita, askari 160 wa Chad waliondoka kwenye ngome zao kaskazini mwa mali kwa sababu kama hizo.