Machafuko yaripotiwa Kinshasa na Goma
Hali ya wasiwasi imeripotiwa leo Jumatatu Januari 19 katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kinshasa wakati sheria ya uchaguzi, ambayo imezua utata, imekua ikitazamiwa kujadiliwa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Sheria hiyo imekua ikitazamiwa kujadiliwa na Baraza la Seneti, baada ya kupitishwa na Bunge.
Imearifiwa kuwa askari polisi wawili na raia wawili wameuawa katika machafuko hayo.
Tangu asubuhi, mkutano wowote unaojumuisha watu wawili hadi kuendelea umekua ukitawanywa na polisi, wakati mwingine polisi imekua ikitumia nguvu na kusababisha vurugu. Polisi imewafyatulia risase waandamanaji.
Kulingana na taarifa zetu za ya awali, mtu mmoja alipigwa risasi pegani katika machafuko hayo, na wakati huu amelazwa hospitalini.
Vyanzo vingine kadhaa vimearifu kwamba watu wengine wamepigwa risase karibu na chuo kikuu cha Kinshasa na katika maeneo mbalimbali ya katikati ya mji ambapo polisi tangu mapema asubuhi imepiga marufuku ya kuandamana.
Wakati huohuo basi moja limechomwa moto karibu na chuo kikuu cha Kinshasa kilomita nne kutoka mjini kati. waandamanaji wenye hasira walizuia barabara kwa kuchoma matairi , huku wakiweka vizuizi vya aina mbalimbali barabarani.
Waandamanaji hao wamekua wakitupia mawe magari yanayopita barabarani. Vijana hao wanalalamikia ukosefu wa ajira, huku wakidai kuondoka madarakani kwa rais Kabila. Visa vya uporaji pia vimeripotiwa.
Wakati hayo yakijiri, machafuko pia yameripotiwa katika mji wa Goma, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Vikosi vya usalana vimelazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi ili kuwatawanya waandamanaji. Miliyo ya risasi na milipuko vimesikika. Watu kadhaa wamearifiwa kukamatwa.