Kabila ataka UN kuingilia kati katika upatanishi wa Wacongo
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Joseph Kabila amependekeza kwenye Umoja wa Mataifa majina ya watu wanne wenye uwezo wa kuhakikisha upatanishi wa kimataifa unafanikiwa kuelezea uchaguzi mkuu mwaka ujao.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Chanzo cha kiserikali nchini humo kimesema kuwa waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Raymond Tshibanda, amewasilisha barua ya Rais Kabila mjini New York kwa Katibu Mkuu wa Umoja huo, Ban Ki-moon.
Kabila amewapendekeza aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan, Rais wa Angola Eduardo Dos Santos, Spika wa Bunge la Senegal Moustapha Niasse, na Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa kwa ukanda wa Maziwa Makuu, Said Djinnit, kupatanisha wakongo katika mazungumzo yaliyoitishwa na Rais huyo.
Kuwepo kwa msuluhishi wa kimataifa ni moja ya masharti yaliyowekwa na chama kikuu cha upinzani nchini DRC cha UDPS cha Bw. Etienne Tshisekedi kwa kushiriki katika mazungumzo hayo.
Tayari vyama kadhaa vya upinzani vimekataa kushiriki katika mazungumzo hayo vikimtuhumu Rais Kabila kuitisha mazungumzo hayo ili kujipa mwanya wa kujiongezea muda ifikapo mwezi Novemba mwaka 2016 rais huyo atakapomaliza mihula yake miwili kwa mujibu wa Katiba.