Ripoti ya jopo la uchunguzi nchini Sudan Kusini lavitaja vikosi vya Serikali kutekeleza mauaji dhidi ya raia
Vikosi wa Sudan Kusini vimewaua watu zaidi ya 50 kwa kuwanyima hewa baada ya kuwahifadhi kwenye makasha maalumu na kuyaweka kwenye eneo la joto, imesema taarifa ya waangalizi wa mkataba wa usitishaji wa mapigano nchi
Imechapishwa: Imehaririwa:
Ripoti hiyo imeongeza kuwa, licha ya makubaliano ya amani ya mwezi August mwaka uliopita, mapigano bado yameendelea na mgogoro huo sasa unahusisha makundi kadhaa ya wapiganaji ambao hawataki kutekeleza mkataba huo wa amani.
Ripoti ya kamati hiyo, imeongeza kuwa mapigano zaidi yanaendelea kushuhudiwa licha ya kutiwa saini kwa mkataba huo wa amani, mapigano ambayo yanadaiwa kutengenezwa na baadhi ya makundi yanayotekeleza mashambulizi ya ulipizaji kisasi.
Ripoti hiyo ya pamoja iliwasilishwa hapo jana kwenye mkutano wa viongozi wa Umoja wa Afrika na kuwekwa wazi kwa uma.
Sehemu ya ripoti hiyo ilipewa kichwa cha habari "Kuhusu mauaji ya raia kwenye jimbo la Unity" eneo ambalo liliorodheshwa kwa mfano wa ukiukwaji wa makubaliano ya mkataba wa amani, ukiukwaji uliotekelezwa na pande zote mbili.
Uchunguzi wa kamati hiyo umebaini kuwa October 22 mwaka uliopita, mwezi mmoja tu baada ya kutiwa saini kwa mkataba wa kusitisha mapigano, watu zaidi ya 50 waliuawa na vikosi vya Serikali kwa kuhifadhiwa kwenye makasha maalumu na hivyo kukosa hewa.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo imesema kuwa, makontena mengi yanatumiwa na vyombo vya usalama nchini humo kuwahamisha wafungwa kutoka eneo moja kwenda eneo jingine, na kwamba eneo la jimbo la Unity, hufikia nyuzi joto zaidi ya 40.
Makosa mengine yaliyoorodheshwa kwenye ripoti hiyo ni pamoja na makosa ya ubakaji, mauaji, utekaji nyara na uporaji wa mali jirani na makambi ya wakimbizi wa Umoja wa mataifa.
Licha ya kutokuwa na taarifa rasmi kutoka jeshi la serikali kuzungumzia ripoti hii, msemaji wa vikosi vya Sudan Kusini amekanusah madai ya ripoti hiyo kwa kile alichodai takwimu nyingi ni za uongo.
Mwezi uliopita, jopo maalumu la wataalamu wa umoja wa Mataifa, lilitaka rais wa Sudan Kusini, Salva Kiir na kiongozi wa waasi Dr Riek Machar wanapaswa kuwekewa vikwazo kutokana na kuhusika kwenye mgogoro huo kwa sehemu kubwa.
Ripoti hii imetolewa huku pande zinazokinzana nchini humo zikishindwa kukubaliana kuunda Serikali ya umoja wa kitaifa licha ya kutakiwa kuwa wameshaunda Serikali hiyo, January 22, kama ilivyokuwa imekubaliwa chini ya mkataba wa amani.