Korea Kaskazini: Kim Jong-un aonekana hadharani
Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un ameonekana hadharani kwa mara ya kwanza tangu mwezi uliopita.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kiongozi mkuu wa taifa la Korea Kaskazini, Kim Jong-un, ameonekana hadharani baada ya kutoonekana sehemu yeyote kwa muda wa siku 40. Kutoonekana kwa kiongozi huyo kulizua hali ya wasi wasi, ambayo haikua kawaida yake. Shirika la habari la serikali ya Corea Kaskazini kimeonesha mapema leo Jumanne asubuhi picha za Kim Jong-un.
Hata hivo kiongozi huyo mkuu wa Korea Kaskazini amekua akitembea akichechemea kwa kutumia fimbo. Hali hii inathibitisha mtazamo wa wachambuzi mbalimbali kwamba kiongozi huyo anakabuliwa na tatizo la miguu. Gazeti la kila siku la Korea Kaskazini limethibitisha Jumatatu Oktoba 13 mwaka 2014 kwamba Kim Jong-un alifanyiwa upasuaji wa vifundo vya miguu na daktari wa Ufaransa katikati ya mwezi Septemba.
Kim Jong-un ameonekana hadharani wakati ambapo hajapata ahueni, na afya yake bado ni tete. Serikali imeonekana kuwa na haraka ya kumuonesha kiongozi huyo hadharani ili kumaliza uvumi wa mapinduzi ya kijeshi na kukosekana kwa utulivu. Pyongyang imesema kiongozi wa taifa hilo, angalau ameonekana hadahrani baada ya kukosekana kwa muda wa siku 40, amekua akijishughulisha na majukumu ya nchi.
Jong Un ameonekana akizungumza na viongozi wa kijeshi akiwa na bakora mkononi iliyomsaidia kutembea wakati akikagua kituo cha Kisayansi jijini Pyongyang.
Juma lililopita kiongozi huyo alikosa kuhudhuria maadhimisho ya miaka 69 ya chama tawala nchini humo na kuzua maswali mengi kuhusu hali yake ya kiafya baada ya kuonekana akitemebea akichechemea.