Waangalizi wa Uchaguzi wa Ukraine wakosoa namna ulivyoendeshwa na kueleza demokrasia haijatendeka

Waangalizi wa Uchaguzi nchini Ukraine wamekosoa vikali namna ambavyo zoezi la uchaguzi huo ulivyoendesha na hata kufikia hatua ya kusema umeonesha kurudi nyuma kwa demokrasia katika nchi hiyo.
Waangalizi wa Uchaguzi huo wakiwemo wale kutoka nchini Marekani wamekiri kusikitishwa na namna ambavyo uchaguzi huo umefanyika na kusema demokrasia haikuchukua nafasi yake ipasavyo.
Malalamiko haya ya Waangalizi wa Uchaguzi nchini Ukraine yanakuja kipindi hiki ambacho Chama Tawala kinachoongozwa na Waziri Mkuu Mykola Azarov kikiongoza kwa kupata wingi wa viti.
Waziri Mkuu Azarov amewahutubia wafuasi wa Chama hicho na kusema walitarajia kupata ushindi huo kutokana na uwezo ambao wanao na wanauhakika wataendelea na sera zao imara katika kuwaleta maendeleo wananchi.
Kwa upande wake Mkuu wa Waangalizi kutoka Taasisi ya Masuala ya Ulinzi na Ushirikiano kutoka Umoja wa Ulaya OSCE Walburga Habsburg Douglas naye amelaani vikali namna ambavyo uchaguzi huo ulivyoendeshwa.
Douglas amekwenda mbali zaidi na kusema matumizi mabaya ya madaraka ndiyo yamekuwa sehemu ya kuharibu uchaguzi huo na hivyo demokrasia ikakosa nafasi yake licha ya uwepo wa utulivu siku ya kupiga kura.
Navyo vyama ambavyo vinamuunga mkono Waziri Mkuu wa zamani Yulia Tymoshenko ambaye anatumikia kifungo kwa kusa la matumizi mabaya ya madaraka yamelalamika uchaguzi huo haukuwa huru wala wa haki.
Upande mwingine ambao umekatishwa tamaa na namna ambavyo uchaguzi huo ulivyoendesha ni ule unaongozwa na Bingwa wa Ngumi Vitaly Klitschko na kueleza uchaguzi huo umeonesha hakuna demokrasia katika Taifa hilo.







MAELEZO
Tuma maoni yako kwa makala haya