Yemen : mashambulizi Sanaa, rais Hadi akimbilia Saudi Arabia
Operesheni “ Dhoruba imara” imeendelea Alhamisi wiki hii katika mji mkuu wa Yemen, Sanaa. Operesheni hii inaendeshwa na mataifa ya Kiarabu kwa lengo la kuwatimua waasi wa Kishia kutoka jamii ya Houthi ambao wanataka kuupindua utawala wa Abd Rabbo Mansour.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa sasa waasi hao wamekua wakiendesha mashambulizi yao katika mji wa Aden, mji ambao kunapatikana bandari kubwa kusini mwa Yemen. Rais wa Yemen ambaye alikua alikimbilia hivi karibuni katika mji huo wa Aden, amewasili Alhamisi Machi 26 nchini Saudi Arabia.
Rais wa Uturuki ameunga mkono operesheni hii inayoendeshwa na mataifa ya Kiarabu nchini Yemen. Katika mahojiano na televisheni ya France 24, Recep Tayyip Erdogan amesema yuko tayari kupeleka msaada wa vifaa vya kijeshi katika operesheni hi inayoendelea.
Milipuko mikubwa ilisikika Alhamisi wiki katika mji wa Sanaa, ambapo muungano unaoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya waasi wa Kishia kutoka jamii ya Houthi umeendelea na operesheni ya kijeshi, huku muungano huo ukiendelea kutekeleza mashambulizi ya angani katika maeneo mbalimbali ya mji wa Sanaa unaoshikiliwa na waasi hao.
Operesheni hii ilianza usiku wa Jumatano kuamkia Alhamisi wiki hii. Mashambulizi yamelenga maeneo muhimu yanayoshikiliwa na waasi, na muungano unaoongozwa na Saudi Arabia umebaini kwamba mashambulizi hayo yalikua yenye mafanikio.
Hata hivyo Iran imepinga mashambulizi hayo katika ardhi ya Yemen, ikibani kwamba ni uvamizi wa majeshi ya kigeni kwa taifa lililo huru. Serikali ya Iran Imeomba operesheni hiyo isitishwe mara moja.