Mashabiki wa Klabu ya Al Ahly ya Misri wasusia mchezo wa fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Esperance

Mashabiki Shupavu wa Klabu ya Al Ahly ya Misri wamejiapiza kutoingia uwanjani kuishangili timu yao kwenye mchezo wa kwanza wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika. Klabu ya Al Ahly ya Misri inatarajiwa kuchuana na Mabingwa Watetezi wa Kombe la Ligi ya Mabingwa Barani Afrika Esperance kwenye michezo miwili ya fainali na kwanza utapigwa katika ardhi ya Misri.
Mashabiki hao wamesema hawatohudhuria kwenye mchezo huo utakaopigwa katika Jiji la Alexandria nchini Misri tarehe nne ya mwezi Novemba kutokana na kuendelea kutaka haki itumike kwa waliopoteza maisha huko Port Said.
Uamuzi huo wa mashabiki wa Klabu ya Al Ahly umekuja kipindi hiki ambacho Wizara ya Mambo ya Ndani nchini Misri ikiruhusu mashabiki elfu ishirini waweze kuhudhuria uwanjani kujionea mtanange huo.
Mashabiki wa Al Ahly wametoa taarifa ikiweka miezi tisa imeshapita tangu kutokea kwa vifo vya zaidi ya watu sabini waliokuwa wanaangalia mchezo kati ya klabu hiyo na Al Masry lakini mashtaka hayajafunguliwa.
Mashabiki hao wenye mapezni makubwa na Al Ahly wamesema hawatokuwa tayari kuhudhuria mchezo wowote katika nchi hiyo hadi pale ambapo haki itakuwa imetendeka dhidi ya waliohusika kwenye vifo vya mashabiki zaidi ya sabini.
Wapenzi wa mpira nchini Misri tangu kutokea kwa vifo vya mashabiki zaidi ya sabini wameshuhudia mchezo mmoja tu na huu kati ya Al Ahly na Esperance utakuwa wa pili katika kipindi cha miezi tisa.
Ligi nchini Misri nayo imesimama kutokana na ghasia ambazo ziliibuka kwenye mchezo wa Ligi kati ya Al Ahly na Al Masry na kuchangia serikali kupiga marufuku michezo yote wakihofia hali ya usalama.







MAELEZO
Tuma maoni yako kwa makala haya