Mapigano makali yameripotiwa kwenye mji wa Benghazi nchini Libya
Mapigano makali yameripotiwa hii leo kwenye mji wa Benghazi mashariki mwa nchi ya Libya, mapigano yanayodaiwa kuwa ni kati ya wapiganaji wa kundi la Ansar al-Shariah na wapiganaji wafiasi wa kiongozi wa zamani wa jeshi, Khalifa Haftar.
Imechapishwa:
Wakazi wa mji wa Benghazi wamethibitisha kusikia milio ya risasi kwenye mji huo, ambapo mbali na mapigano ya Jumatatu ya wiki hii, siku ya Jumapili pia kulishuhudiwa makabiliano kati ya makundi haya hasimu.
Kwenye taarifa iliyotolewa hapo jana na utawala wa Tripoli imesema kuwa watu saba walipoteza maisha na wengine kadhaa wamejerihiwa toka kuanza kwa operesheni za jeshi la nchi hiyo kwenye mji wa Benghazi kuwasaka waasi wa Ansar.
Jeneral Haftar pamoja na wapiganaji wake, ameapa kuyasambaratisha makundi ya waasi wenye silaha mashariki mwa nchi hiyo, makundi ambayo amedai Serikali ya Tripoli imeshindwa kukabiliana nao.
Wakazi wa mji wa Benghazi wameeleza hofu ya usalama wao kwa kile wanachodai kuwa utawala wa Tripoli umeshindwa kabisa kuwadhibiti wapiganaji wenye silaha kwenye mji wa Benghazi na kwenye mji wa Tripoli ambao wamekuwa wakishambulia ofisi za Serikali.
Siku ya Jumapili ndege za kijeshi za Libya zikiongozwa na jenerali Haftar zilishambulia ngome za kundi la Ansar al-Shariah ambao wamepiga kambi mjini Benghazi.
Toka kuangushwa kwa utawala wa Marehemu Kanali Muamar Ghaddafi nchi ya Libya imekuwa ngumu kutawalika kutokana na kuendelea kuzorota kwa hali ya usalama nchini humo kutokana na kukithiri kwa makundi ya wapiganaji wenye silaha.