DRC : waasi wa zamani wa M23 waiomba serikali kuzingatia azimio la Nairobi
Waasi wa zamani wa M23 wameinyooshea kidole cha lawama Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kukwamisha utekelezwaji wa azimio la Nairobi baina ya serikali na waasi hao miezi saba baada ya kutiwa saini azimio hilo.
Imechapishwa:
Waasi hao wanalalamika kuwa azimio la Nairobi iliyowapelekea kuweka silaha chini imetekelezwa kwa asilimia moja tu kwa kile wanachokiona kuwa ni ukosefu wa nia ya dhati kutimiza ahadi hasa ile ya kutoa msamaha kwa waasi wapatikanao katika nchi jirani ya Rwanda na Uganda.
Kulingana na waasi hao, mwezi mmoja kabla ya kufikia makataa ya muda liyowekwa kutekeleza maazimio hayo, hawana uhakika ikiwa muda huo utaongezwa kuruhusu waangalizi kuwafikia waliko, licha ya serikali ya DRC kuahidi kukamilisha mpango huo haraka iwezekanavyo.
Miongoni mwa ahadi hizo ni kutuma ujumbe nchini Rwanda kubaini waliokimbilia nchini humo mwezi March mwaka uliopita, hatua ambayo inalalamikiwa na serikali ya Congo kuwa inakwamishwa na serikali ya Kigali, hasa wakati ujumbe huo ulirudishwa mipakani mwa nchi hizo mbili.
Waasi hao wanakadiriwa kuwa wapatao mia sita nchini Rwanda kulingana na jopo la waangalizi wa Umoja wa Mataifa na ambao 48 tayari wametoweka, na wengine elfu moja mia sita na sabini na nane waliokimbilia nchini Uganda.