Sudani Kusini: mazungumzo yaanza, mapigano yaibuka
Mazungumzo ya amani kuhusu kusitisha vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan Kusini yameanza Jumatatu ya wiki hii mjini Addis Ababa, huku kukishuhudiwa mapigano makali kwenye baadhi ya maeneo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakati huu wajumbe wa mazungumzo haya wakiendelea kuwasili mjini Addis Ababa, makundi ya wapiganaji wenye silaha kwenye jimbo la Upper Nile wamekabiliana na wanajeshi walioasi kwa siku ya pili huku kukishuhidiwa mfanyakazi mmoja wa shirika la misaada akiuawa kutokana na mapigano haya.
Tume ya Umoja wa mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS imesema kwenye taarifa yake, kuwa inaguswa na hali ya kuendelea kushuhudiwa kuzorota kwa usalama nchini humo hasa kwenye miji ya Bunj na jimbo la Upper Nile ambako kuna zaidi ya wakimbizi laki 1 na elfu 25 wanaotoka Sudan.
Kwenye mazungumzo yaliyofunguliwa jana Jumatatu, wapatanishi wa mzozo huo wamewaonya viongozi wanaohasimiana kuhusu hatua ambazo zitachukuliwa dhidi yao iwapo mapigano hayatakomeshwa.
Jumuiya ya maendeleo ya nchi za Afrika mashariki IGAD ambayo ndio inayosimamia mazungumzo haya imeweka makataa ya hadi kufikia tarehe 10 ya mwezi huu kwa viongozi hawa kufikia makubaliano kuhusu serikali ya mpito.
Mazungumzo ya mwisho kati ya rais Salva kiir na aliyekuwa makamu wake wa rais Riek Machar yalikwama mwezi June mwaka huu baada ya kila upande kumtuhumu mwenzake kwa kukiuka mkataba waliotiliana saini.