Joice Mujuru afutwa kazi
Rais wa Zimbabwe Robert Mugabe amemfuta kazi Makamu wa rais Joice Mujuru kwa madai ya kupanga mbinu za kumuua na pia kuhusika na kashfa za ufisadi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Pamoja na Bi Mujuru, rais Mugabe amewafuta kazi pia Mawaziri saba waliokuwa wanaegemea upande Makamu wa rais.
Bi Mujuru amekanusha madai kuwa alikuwa anapanga njama za kumuua rais mugabe mwenye umri wa miaka 90, kama ilivyodaiwa na mke wa rais, Grace Mugabe.
Mbali na kufutwa kazi kama Makamu wa rais, Bi Mujuru ambaye wakati mmoja alioneakna kuwa huenda akawa mrithi wa Mugabe, pia ameondolewa katika Kamati Kuu ya chama cha ZANU-PF.
Miongoni mwa Mawaziri ambao wamefutwa kazi ni pamoja na Waziri wa Usalama wa ndani, Didymus Mutasa, ambaye alikuwa mshirika wa karibu wa Mugabe na Waziri wa Nishati, Dzikamai Mavhaire, mshirika wa karibu wa Bi Mujuru.
Kwa muda wa miezi mitatu sasa rais Mugabe na Makamu wake wa rais, hawajawa na uhusiano mzuri, na kuondolewa kwake katika wadhifa huo hakujawashangaza wananchi wa Zimbabwe.
Haijaelezwa ni nani atakayechukua nafasi ya Bi Mujuru.