Serikali ya mpito bado inasubiriwa Sudan Kusini
Mkutano muhimu uliotarajiwa kati ya Rais wa Sudan Kusini na Kiongozi wa waasi Riek Machar, umegonga mwamba baada ya Kiir kuchelewa kujielekeza mjini Addis Ababa, Ethiopia, ambako mpinzani wake Machar amewasili.
Imechapishwa:
Kutoonekana kwa Kiir kwenye mkutano huo kumegadhabisha Kitengo cha kulinda Usalama cha Umoja wa Mataifa ambacho kinatarajiwa kuiwekea serikali ya Sudan Kusini vikwazo vikali.
Hayo yakiendelea, mjini Juba, Rais Salva Kiir ameamuru vikosi vyake vikomeshe mapigano na waasi na pia amewaita nyumbani wanasiasa kumi walioko uhamishoni na ambao aliwasamehe baada ya kudai kuwa walipanga njama za kuipindua serikali yake mwezi Desemba mwaka 2013.
Kukiwa kumebaki siku saba ili Rais wa Sudan Kusini, Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar waanzishe rasmi serikali ya mpito ya muungano wa kitaifa, wingu la kutatanisha lbado limetanda mjini Addis Ababa, Ethiopia, ambako wawili hao walitarajiwa kukutana kuweka sahihi kwenye makubaliano ya mwisho na ya amani ya kudumu.
Tayari Kiongozi wa waasi Riek Machar amewasili Addis Ababa, lakini Rais Salva Kiir ambaye wapatanishi wa IGAD wamemsubiri, hajawasili Addis Ababa na inasemekana kuwa bado angali Juba, mji mkuu wa Sudan Kusini.
Kinachoendelea kwenye sehemu ya mkutano ni majadiliano ya kina kati ya makundi yanayowawakilisha Rais Kiir na Machar.
Kufikia jioni hii ya Alhamisi, wawakilishi hao wamepitia kwa makini vipengele mbalimbali vinavyohusika na kuleta amani. Wanadiplomasia wanaohudhuria mkutano huo wanaarifu kuwa wawakilishi hao wameshindwa kukubaliana kuunganisha vikosi vya serikali na vya waasi katika serikali ya muungano.