Mkutano wa AU: Bashir akataliwa kuondoka Afrika Kusini
Mkutano wa 25 wa Umoja wa Afrika umefunguliwa Jumapili mwishoni mwa juma hili jijini Johannesburg, nchini Afrika Kusini. Zaidi ya marais hamsini wamehudhuria mkutano huo.
Imechapishwa:
Hata hivyo mgawanyiko umejitokeza, kwani Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa kivita (ICC) imeiomba serikali ya Afrika Kusini kumzuia rais wa Sudan Omar al-Bashir, ambaye anatuhumiwa na Mahakama hiyo makosa ya uhalifu dhidi ya binadamu na mauaji ya kimbari katika vita viliyotokea Darfur.
Omar al-Bashiri ameshiriki pia katika mkutano huo wa Umoja wa Afrika. Mahakama ya Afrika Kusini, imeombwa na shirika lisilo la kiserikali la Southern Africa Litigation Center, kumzuia rais wa Sudan ili asiwezi kuondoka nchini humo, angalau mpaka kesho.
Shirika hilo limeiomba Mahakama ya Afrka Kusini kumzuia rais Omar al-Bashir na kumsafirisha hadi kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa kivita (ICC). Kufuatia ombi hilo, Mahakama ya Pretoria imemzuia rais wa Sudan kutothubutu kuondoka nchini Afrika Kusini mpaka vyombo vya sheria vitoe uamzi wake wa mwisho.
Kesi hiyo imeahirishwa kusikilizwa hadi kesho Jumatatu asubuhi kwa ombi la wakili wa serikali wa Afrika Kusini, ambaye anahitaji kuandaa hoja yake kwa ajili ya kikao cha pili.
Licha ya kuahirishwa kwa kesi hiyo, jaji ametoa dhamana kubwa kwa shirika hilo lililofungua mashtaka. Waziri ya mambo ya ndani wa Afrika Kusini ametakiwa kufuatilia kwa karibu maeneo yote hususan mipaka ambapo rais Omar al-Bashir anaweza kupitia kwa kuondoka nchini Afrika Kusini usiku wa leo Jumapili. Maafisa wanaofanya ukaguzi kwenye mipaka wanapaswa kupewa taarifa mara moja ili kuzuia jaribio lolote la kutoroka kwa rais wa Sudan.
Ushindi wa kwanza
Uamuzi huu ni ushindi wa kwanza kwa shirika lisilo la kiserikali la SACL. Wawakilishi wa shirika hilo wana matumaini kwamba vyombo vya sheria vya Afrika Kusini vitatoa ishara ya nguvu kuonyesha kuwa Afrika Kusini inaheshimu sheria za kimataifa na kwamba serikali inaheshimu majukumu yake ya kikatiba.