Rais wa Chad, aonya viongozi wenzake kushindwa kuchukua hatua, ataka waache kuwa na maneno mengi kuliko vitendo
Mkutano wa 26 wa wakuu wa nchi za Umoja wa Afrika, AU, siku ya Jumapili wamemaliza mkutano wao wa siku mbili huku wakishindwa kuchukua hatua katika nchi zenye migogoro ikiwemo Burundi.
Imechapishwa:
Mwishoni mwa juma mjadala mkubwa ulikuwa ni kuamua iwapo Umoja huo uidhinishe kupelekwa kwa wanajeshi wa kulinda amani nchini Burundi au la, mjadala ambao hata hivyo ulimalizika kwa viongozi hao kushindwa kuafikiana kupelekwa kwa wanajeshi hao.
Viongozi hao wanasema kuwa hawawezi kupeleka wanajeshi wa kulinda amani nchini Burundi, ikiwa viongozi wenyewe wa Burundi, hawataka kuwapokea kwa kile inachosisitiza kuwa hakuna haja ya kupelekwa kwa wanajeshi hao.
Badala yake viongozi hao wamekubaliana kutuma mjumbe maalumu wa Umoja huo, kwenda nchini Burundi kukutana na Serikali pamoja na upande unaopinga muhula watatu wa rais Nkurunziza.
Mjumbe huyo aatakuwa na jukumu la kuhakikisha mazungumzo zaidi yanafanyika kutafuta suluhu ya mzozo wa kisiasa nchini humo, hatua ambayo hata hivyo mjumbe huyo anaweza asifanye kitu kwakuwa mjumbe wa awali alishindwa kufikia muafaka na pande zinazokinzana nchini humo.
Uamuzi huu wa viongozi wa Umoja wa Afrika, umetokana na Ibara ya 4 (h) ya mkataba wa AU unaohusu kupelekwa kwa wanajeshi wa kulindwa amani, ambapo viongozi hao wanapaswa kuchukua hatua hiyo ikiwa kuna ulazima wa kufanya hivyo kama vile sababu za kivita, mauaji na makosa ya uhalifu dhidi ya binadamu.
Na zaidi mkataba huo unataka wanajeshi wapelekwe ikiwa nchi mwanachama imeridhia kupelekwa kwa wanajeshi wa kulinda amani, suala ambalo nchi ya Burundi imekataa kupelekwa kwa wanajeshi hao.
Umoja wa Mataifa umeonya kuwa nchi ya Burundi iko kwenye hatari ya kutumbukia kwa mara nyingine kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe kama vile vya mwaka 1993-2006, ambapo mpaka sasa mamia ya raia wameuawa toka mwezi April 2015, wakati rais Pierre Nkurunziza alipotangaza kuwania urais kwa muhula wa tatu mfululizo.
Watu zaidi ya laki mbili na elfu thelathini raia wa Burundi wamekimbia makazi yao kutokana na vurugu za kisiasa zinazoendelea kushuhudiwa nchini humo.
Hata hivyo mkuu wa baraza la usalama la Umoja wa Afrika, Smail Chergui amesema kuwa licha ya wanajeshi hao kutopelekwa kwa wakati huu, amoengeza kuwa katika siku zijazo huenda wanajeshi hao wakapelekwa kulingana na jinsi hali itakavyokuwa.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mkutano huo, waziri wa mambo ya nje wa Burundi, Alain Aime Nyamitwe amesema kuwa Serikali yao imeridhishw ana uamuzi wa wakuu hao wa nchi, na kwamba Serikali iko tayari kuendelea na juhudu za mazungumzo ili kufikia suluhu.
Katika hatua nyingine amehoji ni kwanini mjumbe wa Umoja wa Afrika anatumwa kwamara nyingine kwenda Bujumbura, wakati kila mtu anajua kila kitu kinachoendelea kwa sasa.
Kwa upande wake mwenyekiti mpya wa Umoja huo, rais wa Chad, Idriss Deby akizungumza baada ya kuchukua wadhifa huo kutoka kwa rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe, amewaonya viongozi wenzake kwa kushindw akuchukua hatua, na badala yake wamekuwa na maneno mengi zaidi kuliko vitendo.
Rais Deby ameongeza kuwa taasisi ya Umoja wa Afrika imeendelea kufabnya kazi kama miaka 20 iliyopita, ambapo wanakutana kila mara, kuzungumza kwa muda mrefu na kuandika makaratasi mengi lakini wanashindwa kuchukua hatua na wakati mwingine hawajigusi kabisa.
deby anataka wakuu wa nchi wanapokutana na kuridhia mikataba mbalimbali, wawe wanatekeleza na kuchukua hatua stahiki hasa kwenye nchi zenye migogoro ili kunusuru malefu ya raia wanaoendelea kuuawa kwasababu viongozi wao wanashindwa kuchukua hatua.