Gambia: Rais Adama Barrow ateua mkuu mpya wa majeshi
Rais wa Gambia, Adama Barrow amemfuta kazi mkuu wa majeshi ya nchi hiyo, Jenerali Ousman Badjie, wakati huu akiendelea kufanya mabadiliko makubwa ya maofisa wa idara za usalama waliokuwa wanahusishwa na utawala wa mtangulizi wake.
Imechapishwa:
Nafasi ya Badjie imechukuliwa na Jeneralu Masanneh Kinteh, aliyewahi kuwa balozi wa nchi hiyo kwenye nchi ya Cuba na mshauri wa masuala ya kijeshi wa Barrow toka mwezi January mwaka huu.
Wakati akichukua wadhifa huo kutoka kwa Badjie, Kinteh amewaambia waandishi wa habari katika makao makuu ya jeshi mjini Banjul: "Kipaumbele changu cha kwanza kabisa kama mkuu wa majeshi ni kurejesha imani kwa vikosi na maadili."
Ameongeza kuwa anataka kurejesha uhusiano mzuri kati ya raia na jeshi baada ya uhusiano huo kuwa umezorota kutokana na hali ya kisiasa iliyokuwepo.
Taarifa zinasema kuwa Badjie ambaye anatajwa kuwa atapewa wadhifa mwingine nje ya nchi, amekabidhi gari analotumia pamoja na nyaraka nyingine muhimu za kijeshi kwa mrithi wake.
Rais Barrow alikula kiapo Februari 18 mwaka huu, mwezi mmoja tu baada ya kuwa ameapishwa nje ya nchi yake nchini Senegal baada ya kutokea sintofahamu ya kimadaraka kati yake na Yahya Jammeh.
Jammeh alikataa kuondoka madarakani baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa mwezi Desemba mwaka jana, lakini alikubali kuondoka kwenda kuishi uhamishoni Januari 21 mwaka huu kufuatia makubaliano aliyofikia na wakuu wa nchi za Afrika Magharibi.
Barrow aliwaambia raia wake kuwa, atawachukulia hatua na kufanya uchunguzi kuhusiana na matukio ya unyanyasaji wa haki za binadamu na kwamba polisi wote waliohusika pamoja na wanajeshi watashtakiwa kwa mujibu wa sheria.
Barrow aliahidi pia kuunda tume ya haki za binadamu ambayo itapewa jukumu la kuchunguza visa hivyo.