Aliekuwa makamu wa rais kumrithi Mugabe
Aliyekuwa makamu wa rais wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa ambaye alifutwa kazi wiki tatu zilizopita na kutoroka nchi hiyo kufuatia vitisho vya kifo , anatazamia kurejea nchini leo Jumatano mchana, siku moja baada ya rais Robert Mugabe kujiuzulu, na kuongoza Zimbabwe kwa muda kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka ujao.
Imechapishwa:
Emmerson Mnangagwa anatazamia kuchukua hatamu ya uongozi wa nchi baada ya kuteuliwa katika mkutano wa hadhara wa chama cha Zanu-PF siku ya Jumapili kuongoza chama hicho tawala.
Kulingana na katiba ya nchi ya Zimbabwe rais anapojiuzulu makamu wake ndio anachukua nafasi yake hadi uchaguzi mpya.
Bw. Mnangagwa atatawazwa kesho Alhamisi na hivyo kuanza rasmi majukumu ya uongozi wa taifa la Zimbabwe, baada ya miaka 37 ya uongozi wa Robert Mugabe.
Maelfu ya raia wa Zimbabwe walimiminika katika mitaa ya miji mbalimbali baada ya tangazo la kujiuzulu kwa rais Robert Mugabe.
Mchakato wa kumtimua Rais Robert Mugabe ulikua ulianza bungeni saa chache kabla ya hatua yake ya kujuzulu.
Raia wa Zimbabwe wanaamini kuwa, kujiuzulu kwa Mugabe ni mwamko mpya kwa nchi yao kiuchumi na kisiasa.
Emmerson Mnagangwa, anatarajiwa kuongoza kwa muda kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka ujao.
Jeshi nchini humo lilianzisha mchakato wa kukosa imani na uongozi wa Mugabe baada ya mkewe Grace, kuonekana kuingilia uongozi wake.