Ethiopia yataka mzozo na majirani zake kutatuliwa na wao wenyewe
Ethiopia imesema haitoruhusu watu wa nje kushirikishwa kwenye mazungumzo mapya ya kujaribu kupata suluhu kuhusu mzozo wa matumizi ya Mto Nile.
Imechapishwa:
Mvutano huo umekithiri na kulazimu Marekani kuingilia kati ingawaje Ethiopia imekuwa ikidai inashinikizwa kusaini mkataba ambao hautazingatia maslahi ya raia wa nchi hiyo.
Ethiopia inajenga bwawa kubwa la kuzalisha umeme, mradi unaopingwa na Misri inayosema unahatarisha maisha ya watu wake ambao watakosa maji.
Kuanza kwa zoezi la kujaza bwawa kubwa la kuzalisha umeme umeme la Renaissance kwenye Mto wa Nile, hatua iliyotangazwa wiki iliyopita na Ethiopia, kunaendelea kuzua mvutano na nchi jirani.
Mwezi uliopita Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres aliziataka Ethiopia, Sudani na Misri kuwa na "uvumilivu" katika juhudi zao za kufikia makubaliano, wakati mazungumzo ya Washington yalisitishwa tangu mwezi Februari.
Katikati ya mzozo huo ni mpango wa kujaza bwawa hilo kuu, Ethiopia inataka kutekeleza mpango huo kwa kipindi cha miaka sita, Misri ikipendekeza muda wa miaka kumi ikihofu mradi huo utafanya Ethiopia kudhibiti maji ya mto Nile.
Mradi huu unaotarajiwa kuanza kuzalisha umeme kuanzia mwaka 2022 utagharimu dola bilioni nne za Kimarekani.
Ni mradi mkubwa lakini umesababisha pia mgogoro wa kidiplomasia kati ya Misri na Sudan kwani nao wanategemea maji ya mto Nile.