Wanajeshi watatu wa Umoja wa Mataifa, wauawa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati
Watu wasiofahamika waliokuwa wamevalia sare za kijeshi wameuawa wanajeshi watatu wa Umoja wa Mataifa walio kwenye kikosi cha kulinda Amani nchini humo, kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Umoja wa Mataifa unasema wanajeshi waliouawa ni kutokea nchini Burundi, na waliuawa siku ya Ijumaa katika eneo la Dekoa.
Ni mauaji ambayo yametokea saa chache baada ya muungano wa waasi kutangaza kufuta uamuzi wao wa kuacha mapambano dhidi ya vikosi vya serikali na vile vya Umoja wa Mataifa.
Taarifa ya kina haijaeleza kuhusu kuuawa kwa wanajeshi hao, lakini imebainika kuwa wanajeshi wengine wawili walijeruhiwa.
Mauaji haya yametokea wakati wananchi wa taifa hilo wanapojiandaa kupiga kura siku ya Jumapili, uchgauzi ambao unaoelezwa kama kipimo cha demokrasia katika taifa hilo ambalo limekosa utulivu tangu mwaka 2013.
Siku ya Jumamosi, Mahakama ya Katiba iliamua kuwa uchaguzi huo utaendelea kama ilivyopangwa baada ya makundi ya waasi kutaka uchaguzi huo kuahirishwa.
Rais Faustin-Archange Touadera, anayetafuta muhula mwingine, anapewa nafasi kuba ya kushinda dhidi ya wapinzani wake 17.