Mauaji ya Ghislaine Dupont na Claude Verlon: Kiongozi wa kundi la wauaji auawa
Paris imethibitisha kifo cha Baye Ag Bakabo, mkuu wa kundi lililoteka nyara wenzetu Ghislaine Dupont na Claude Verlon Novemba 2, 2013 huko Kidal kaskazini mwa Mali.
Imechapishwa:
Habari hiyo imekuwa ikizungumzwa tangu Jumatano, Juni 9, lakini wakati huo haikuwa rasmi. Ndugu kadhaa wa familia ya Baye Ag Bakabo walikuwa wametangaza kifo chake kwenye mitandao ya kijamii, lakini kikosi cha Barkhane na ikulu ya Elysee, wakati huo, walikuwa hawajathibitisha kifo chake.
Katika taarifa yake, Waziri wa Majeshi Florence Parly ameeleza kwamba "Juni 5 mchana, kikosi cha Barkhane kiligundua shambulio lililokuwa likiandaliwa dhidi ya kambi ya Umoja wa Mataifaya huko Aguelhok kaskazini mwa Mali.
Operesheni ya nguvu wakati huo ilizinduliwa dhidi ya kundi la kigaidi ambalo lilikuwa likiandaa kurusha kombora kwenye kambi hiyo ya Minusma (UN) iliyokuwa ikikaliwa na kikosi cha wanajeshi wa Chad. Operesheni hii iliwezesha magaidi wanne kuangamizwa. Baye Ag Bakabo, kiongozi wa kigaidi anayedaiwa kuhusika katika utekaji nyara na mauaji ya Ghislaine Dupont na Claude Verlon, waandishi wa habari wa RFI, huko Kidal Novemba 2, 2013. "
Kulingana na vyanzo vyetu, Baye Ag Bakabo aliuawa karibu na mji wa Aguelhok alikokuwa tangu mwanzoni mwa wiki hii. Pamoja an kundi lake la Katiba, alikuwa akijiandaa kushambulia kambi ya jeshi ya vikosi vya Mali, hapo ndipo agizo lilitolewa na jeshi la Ufaransa kumuangamiza.