Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya DRC na makundi ya waasi kufanyika Novemba 21
Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya DRC na makundi ya waasi, yanayolenga kuleta utulivu Mashariki mwa nchini hiyo, yaliyokuwa yamepangwa kufanyika jijini Nairobi, tarehe 16 mwezi huu, sasa yatafanyika tarehe 21, wakati huu mapigano yakiendelea kati ya waasi wa M23 na wanajeshi wa FARDC.
Imechapishwa:
Tarehe hii mpya, imetangazwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki, wakati msuluhishi wa Jumuiya hiyo, rais wa zamani wa Kenya, Uhuru Kenyatta akizuru jijini Kinshasa kwa siku mbili, kuendeleza mchakato wa kidiplomasia ili kupata suluhu.
Ziara hii inakuja pia wakati huu mapigano kati ya jeshi la DRC na waasi wa M23 yakiendelea, umbali wa kilomita 25 hadi 30 kutoka mjini wa Goma, makao makuu ya mkoa wa Kivu Kaskazini.
Ripoti zinasema mapigano kwa sasa yanaendelea katilka êneo la Mwaro, na ripoti za kiusalama zinawashtumu waasi wa M 23 kutekeleza mauaji ya raia na wanajeshi wa DRC.
Vyanzo vingine, vinasema, mapigano makali yaliendelea kushuhudiwa katika êneo la Kibumba, kufikia jana jioni na yameendelea siku moja baada ya Kenya kuanza kutuma vikosi vyake mjini Goma.
Mapigano yanayoendelea, yamesababisha hali ya wasiwasi kai ya DRC na Rwanda, na tangu mwaka huu, Kinshasa imeendelea kuishtumu Kigali kuwaunga mkono waasi, hao, madai ambayo imeendelea kukanusha.