Jeshi la Uganda katika shinikizo DRC
NAIROBI – Vyanzo vya habari nchini Uganda, vinasema kwamba jeshi la nchi hiyo liko katika shinikizo kubwa kuhusu vita dhidi ya makundi ya waasi mashariki mwa DRC, wakati huu pia vikosi vya Jumuiya ya Afrika Mashariki vikinyooshewa kidole kwa kushindwa kuwakabili vilivyo waasi wa M23.
Imechapishwa:
Cheza - 00:59
Taarifa inasema kuwa imekuwa vigumu kwa wanajeshi wa jumuiya ya Afrika mashariki kukabiliana moja kwa moja na waasi wa M23 kutokana na kwamba huenda wanaungwa mkono na baadhi ya nchi wanachama, hasa taifa la Rwanda ambalo limetuhumiwa mara kadhaa.
Taifa la Uganda wakati huu linasemekana kuwa chini ya shinikizo za kuwatuma wanajeshi wake katika mkoa wa Kivu Kaskazini kukabiliana na waasi M23, lakini huenda hilo lisifanyike kutokana na kwamba litaibua tofauti za maslahi kwani tayari wanajeshi wa Kenya wamepiga kambi katika mji wa Goma, ila bado waasi wa M23 wanaendelea kuchukuwa udhibiti wa baadhi ya miji.
Habari zaidi zinasema kuwa Uganda itawatuma wanajeshi wake UPDF 2, 500 nchini DRC kukabiliana na waasi wa M23, lakini pia taifa hilo linatathimini athari oparesheni hiyo kwa uhusiano wake na taifa jirani la Rwanda ambao DRC inatuhumu kuunga mkono waasi wa M23, hasa ikizingatiwa uhusiano wa Uganda na Rwanda umeanza kuimarika hivi karibuni