Sierra Leone : Julius Maada Bio anaongoza kwa mujibu wa matokeo ya awali
Nairobi – Rais wa Sierra Leone Julius Maada Bio, anaongoza kwenye matokeo ya uchaguzi wa urais ya Jumamosi Iliyopita, imesema tume ya uchaguzi.
Imechapishwa:
Cheza - 01:11
Katika asilimia 60 ya kura zilizohesabiwa, tume ya uchaguzi imesema, rais Maada Bio amejizolea asilimia 55 ya kura ,hii ikiwa ni kura milioni moja ,elfu sitini ,mia sita sitini na sita huku mpinzani Wake wa karibu Samura Kamara akiwa kura laki saba elfu tisini na tatu mia saba hamsini na moja ,ambayo ni asilimia 41 ya kura zote.
Hata hivyo chama cha upinzani All People's Congress (APC), kimepinga matokeo hayo na kusema si ya wazi huku ikiituhumu tume ya uchaguzi kwa kukosa kuwajibika ipasavyo na kuwashirikisha wadau wote.
Upinzani umedai tume ya uchaguzi haikutoa taarifa muhimu kuhusu vituo vya kupigia kura na wilaya zinazotokea kura zilizohesabiwa.
Waangalizi wa umoja wa Ulaya pia imesema tume ya uchaguzi kutokuwa wazi imefanya matokeo haya na mchakato wote kutoaminika,huku wakilaani vurugu zilizoshuhudiwa katika baadhi ya maeneo na pia makao makuu ya chama cha upinzani siku ya Jumapili.
Mwenyekiti wa tume hiyo Mohammed Kenewui Konneh amesema matokeo rasmi yanatazamiwa kutangazwa ndani ya saa 48.