Makumi ya watu hawajulikani walipo baada ya maporomoko ya ardhi kusini magharibi mwa China
Takriban watu 47 hawajulikani waliko leo Jumatatu baada ya maporomoko ya ardhi kuripotiwa katika mkoa wa Yunnan kusini magharibi mwa China, vyombo vya habari vya serikali vimeripoti. Mamia ya wakaazi wamehamishwa haraka, kazi ya kuwatafuta walionusurika inaendelea.
Imechapishwa:
Maporomoko ya ardhi yamewazika watu 47 asubuhi ya Jumatatu Januari 22 katika eneo la mbali na milimani katika mkoa wa Yunnan, kusini magharibi mwa China, vyombo vya habari vya serikali vimesema, bila kutangaza vifo vyovyote katika eneo hilo.
Mkasa huo ulitokea saa 5:51 asubuhi (saa 9:51 GMT siku ya Jumapili) katika kijiji cha Liangshui, kilichoko katika kaunti ya Zhenxiong, na "watu 47 kutoka kaya 18 walizikwa," shirika la habari la New China limesema.
"Zaidi ya wakazi 200 wamehamishwa kwa haraka, wachimbaji kumi, magari ya zima moto 33 na waokoaji zaidi ya 200 walihamasishwa kwa shughuli za utafutaji," ilisema televisheni ya umma CCTV.
Video iliyorushwa hewani na shirika la habari la New China inaonyesha karibu wazima moto kumi waliovalia suti za rangi ya chungwa na helmeti wakisonga mbele kwenye kile kinachoonekana kuwa matofali ya zege yaliyoporomoka na uchafu mwingine.
Picha zilizochapishwa na watumiaji wa mtandao wa kijamii wa China wa Douyin zinaonyesha kijiji cha mlimani kilichofunikwa na theluji na nyumba zilizozikwa kwa kile kinachoonekana kuwa maporomoko ya ardhi.
Maporomoko ya ardhi ya mara kwa mara
Yunnan ni mkoa wa milimani, unaokaliwa na makabila mengi na ambao bado ni mojawapo ya majimbo maskini zaidi nchini China.
(Pamoja na AFP)