Senegal: Kauli ya rais Sall kuhusu tarehe ya uchaguzi yapingwa
Nairobi – Nchini Senegal, muungano wa mashirika ya kiraia zaidi ya 40, umekataa kauli ya rais Macky Sall kuwa tarehe ya uchaguzi wa urais ulioahirishwa haiwezi kupangwa kwa sasa, na unasisitiza kuwa, ni lazima ufanyike kabla ya tarehe 2 Aprili, wakati muhula wake utakapofika mwisho.
Imechapishwa:
Kauli hii imekuja baada ya rais Sall hapo jana kupitia mahojiano maalum ya Televisheni, kuahidi kuwa ataondoka madarakani kufikia Aprili tarehe mbili, lakini hakueleza ni lini uchaguzi utafanyika, baada ya shinikizo za ndani na nje, kutaka uchaguzi ulioahirishwa kufanyika haraka iwezekanavyo.
Sall alisisitiza kuwa, tarehe ya uchaguzi huo, inaweza kutangazwa tu baada ya mazungumzo ya kisiasa na wadau wengine, yaliyopangwa kuanza siku ya Jumatatu.
Aidha, Sall ameahidi kutafakari uwezekano wa kuwaachia huru wanasiasa waliofungwa wakiongozwa na Ousmane Sonko aliyekuwa ameonesha nia ya kuwania urais lakini akazuiwa pamoja na Bassirou Diomaye Faye.
Aar Sunu Election, muungano wa mashirika ya kiraia, umesema kauli ya rais Sall haiwezi kuaminika na ni mbinu ya kuchelewesha zaidi uchaguzi huo ili aendelee kukaa madarakani.
Baada ya kuahirishwa kwa uchaguzi huo kutoka Februari hadi Desemba, Senegal iliingia kwenye machafuko na kusababisha maafa ya watu watatu na mamia kujeruhiwa, na baadaye Mahakama ya Katiba ikafuta tangazo la kuahirishwa kwa uchaguzi huo na kusema ni kinyume cha katiba.