Togo: Kampeni za wagombea viti vya ubunge zimeanza rasmi leo
Kampeni za uchaguzi wa wabunge uliopangwa kufanyika tarehe 29 mwezi huu nchini Togo, zimeanza leo wakati huu kukiwa na sintofahamu ya kisiasa kufuatia mchakato wa kuifanyia marekebisho katiba ya nchi hiyo.
Imechapishwa:
Kwa wiki mbili, kampeni hizo zitaendelea, kuelekea uchaguzi huo, ambapo wananchi wa Togo watapata fursa ya kuwachagua wawakilishi wake.
Uchaguzi huo ulikuwa umepangwa kufanyika wiki hii lakini ukaahirishwa na rais Faure Gnassingbè, baada ya kuzuka kwa mvutano wa kisiasa baada ya bunge kupitisha mabadiliko ya katiba, kubadilisha mfumo wa uongozi ambapo wabunge ndio watakaokuwa wanamchagua rais.
Vyama vya upinzani vimepinga mabadiliko hayo na viliitisha maandamano siku ya Ijumaa na Jumamosi, kupinga hatua hiyo ya wabunge wakisema ni mpango wa rais Gnassingbè, kuendelea kusalia madarakani.
Viongozi wa dini na mashirika ya kirai, pia yamemtaka rais Gnassingbè, kutotia saini mabadiliko hayo, na kuitisha mazungumzo ya kitaifa.