Pata taarifa kuu
ZIMBABWE

Upinzani nchini Zimbabwe wakashifu baraza la mawaziri

Upinzani nchini Zimbabwe umekosoa baraza jipya la mawaziri lililotangazwa na rais Robert Mugabe, ukisema kiongozi huyo ameteua watu walewale ambao wameshindwa kuleta mabadiliko nchini humo.

Rais wa Zimbabwe, Robert Gabriel Mugabe
Rais wa Zimbabwe, Robert Gabriel Mugabe Reuters
Matangazo ya kibiashara

Chama kikuu cha upinzani nchini humo cha MDC-T kimesema kuwa mawaziri walioteuliwa kuunda baraza jipya la mawaziri toka chama tawala cha ZANU-PF lina sura zilezile za wazee na viongozi ambao wameshindwa kuleta mabadiliko nchini Zimbabwe.

Kwenye mahojiano maalumu na rfikiswahili msemaji wa MDC, Douglas Mwanzora amesema hakuna mabadiliko ambayo yanatarajiwa kwenye Serikali ya sasa na kwamba uteuzi wa mawaziri haukuzingatia vigezo na uwezo wa watu katika kuleta mabadiliko nchini humo.

Mwonzora ameongeza kuwa wengi wa mawaziri wanaounda baraza jipya la mawaziri walikuwepo kwenye Serikali ya umoja wa kitaifa iliyomaliza muda wake na wengi walishindwa kuleta mabadiliko ambayo wananchi wa Zimbabwe wanayataka.

Wakati wa sherehe za kuapishwa kwa mawaziri hao, rais Mugabe ameahidi kuleta mabadiliko kwenye Serikali yake na kudai kuwa atayashughulikia makampuni ya kigeni yaliyoko nchini humo kukubali uwekezaji wa asilimia 51 kubaki kwa Zimbabwe na wao kuchukua asilimia 49.

Rais Mugabe amesema anataka kuona mabadiliko nchini mwake na kumtaka kila waziri aliyemchagua kutekeleza kile ambacho wananchi waliwapa dhamana wakati wa kempeni za urais.

Baraza jipya la mawaziri limejaa nyuso za viongozi waliopigania uhuru wa Zimbabwe na watu ambao ni wafuasi wa damu wa chama tawala cha ZANU-PF.

Katika hatua nyingine, aliyekuwa waziri wa sheria, Patrick Chinamasa ameteuliwa kuongoza wizara ya uchumi na biashara akiwa na jukumu la kuhakikisha uchumi wa Zimbabwe unaimarika.

Kiongozi mkuu wa upinzani nchini humo, Morgan Tsvangirai ameendelea kusisitiza kuwa uchaguzi wa mwaka huu uligubikwa na mizengwe na ushindi wa rais Mugabe haukuwa halali.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.