Mtu mwenye silaha awaua watu watatu Copenhagen
Watu watatu wameuawa nchini Denmark, na wengine kujeruhiwa baada ya mtu aliyekuwa amejihami kwa bastola kuwafwatulia risasi watu katika jumba la kufanyia biashara jijini Copenhagen.
Imechapishwa:
Picha kutoka eneo la tukio zimeonyesha wazazi wakiwabeba watoto wao na kukimbia kutoka jumba hilo huku magari ya kuwabeba wagonjwa yakiwakimbiza majeruhi hospitalini huku ripoti za awali zikionesha kuwa watu watatu wamethibitishwa kuuawa.
Mkuu wa polisi jijini Copenhagen Soren Thomassen, amesema mshukiwa mwenye umri wa miaka 22 amekamatwa , na wanaendelea na uchunguzi kubaini ni kwanini alitekeleza tukio hilo.
Aidha, Polisi imethibitisha kuwa inachunguza video zilizochapishwa kwenye mtandao zilizodai kuonyesha mshukiwa akiwa na silaha na kujinyooshea bunduki kichwani.
Shambulio hili limejiri siku mbili tu baada ya kuanza kwa mbio za baiskeli za Tour De France, ambazo zilianzia jijini Copenhagen ambapo wapangaji wa mashindano hayo wametuma risala zao kwa waathiriwa na familia zao.
Februari mwaka 2015, watu wawili waliuawa na watano kujeruhiwa katika jiji hilo katika tukio lingine la ufyatuaji lililoelezwa kuwa la kigaidi.