Marekani yaionya Urusi kuhusu Ukraine
Makamu wa rais wa Marekani Joe Biden ameionya Urusi kwa kile alichokiita kuingilia masuala ya ndani ya Ukraine na kutaka kuigawa nchi hio baada ya kuunga mkono wanaharakati wanaounga mkono wa kujitenga na Ukraine na kujiunga na Urusi.
Imechapishwa:
Kwa upande wake kaimu rais wa Ukraine Olexandre Tourtchinov amebaini kwamba wanaharakati wanaounga mkono wa kujitenga, wamevuka “eneo la hatari”, na kutangaza kuanzisha kwa mara nyingine operesheni “dhidi ya ugaidi” mashariki mwa taifa hilo, operesheni ambayo ilisitishwa kabla ya pasaka, baada ya kugundua miili ya watu wawili waliyouawa, ambapo mmoja miongoni mwa watu hao anasadikiwa kuwa mbunge wa jimbo kutoka chama cha Ioulia Timochenko, Batkivchtchina.
Kwa mujibu wa Tourtchinov, matumaini ya kupatikana kwa amani baada ya kutia saini makubaliano ya kimataifa mjini Geneva alhamisi iliyopita yameonekana kufifia, baada ya wanaharakati wanaounga mkono kujitenga “kudhibiti jimbo la Donetsk”.
Akikamilisha ziara yake Joe Biden ameionya nchi ya urusi kuacha mara moja vitendo vya kuingilia masuala ya ndani ya nchi ya Ukraine kwani haina haki ya kufanya hivyo.
Kauli hiyo ya Joe Biden imekuja wakati huu urusi ikiwa na maelfu ya wanajeshi wake kwenye mpaka wake upande wa mashariki mwa Ukraine hatua ambayo inapingwa vikali na jumuiya ya kimataifa.
Biden amesisitiza kuwa Marekani na washirika wake kamwe hawatarusu Urusi kuingilia Ukraine katika mambo yake ya ndani kwani ni kinyume na sheria za kimataifa.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Marekani John Kerry alimuelezea jana mwenyeji wake wa Urusi Sergueï Lavrov wasiwasi wake juu ya ukosefu wa hatua madhubuti ambazo zinapaswa kuchukuliwa na Urusi ili kurejesha hali ya utulivu nchini Ukraine.
Katika hatua nyingine Marekani ambayo inaituhumu Urusi kuendelea kuchochea vurugu nchini Ukraine, imetangaza kutuma wanajeshi 600 kwa ajili ya mazoezi ya kijeshi katika nchi jirani ya Poland, na imeahidi kuiwekea Urusi vikwazo zaidi.
“Muda umewadia sasa kuachana na maneno na kuanza kutekeleza vitendo (…) Tunapaswa kujadili hatua ambazo zinapaswa kuchukuliwa haraka, muda umehesabiwa”, Biden amesema akisisitiza akiwa pamoja na waziri mkuu wa Ukraine Arseni Iatseniouk walipokua wakitoa tangazo mbele ya vyombo vya habari mjini Kiev.
Biden ameitaka Moscow kuyaondoa majeshi yake yanayoendelea kukusanyika kwenye mpaka, na kuacha kuunga mkono watu wanaojificha nyuso na kuvaa sare zisiyokua na ishara yoyote ya jeshi.
Biden ameionya Urusi kwamba iwapo itaendelea na chokochoko zake, itachukuliwa hatua kali ikiwemo kutengwa.