Sudani Kusini: UN yaonya pande zinazozozana
Ujumbe wa baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa umewaonya viongozi wanaopingana nchini Sudan kusini leo jumatano kuwa watakabiliwa na vikwazo iwapo vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyolisukuma taifa hilo changa katika ukingo wa janga la njaa havitakoma.
Imechapishwa:
Misimamo ya makundi mawili yanayohusika katika mgogoro unaoendelea nchini Sudani Kusini tangu mwezi Desemba, inaonesha kufifia kwa matumaini ya amani, amesema balozi wa Uingereza kwenye Umoja wa Mataifa, Mark Lyall Grant, akiwa ziarani Juba.
“Tumekutana kwa mazungumzo na rais wa Sudani Kusini, Salva Kiir, na makamu wake wa zamani, Riek Machar, hakuna hata mmoja aliyetuthibitishia mchango wake kwa jitihada za mchakato wakumaliza mzozo unaoendelea aidha kuhusu mkataba wa haraka wa kusitisha machafuko katika mazungumzo yanayoendelea mjini Addis Abeba, nchini Ethiopia.
Kwa upande wake balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Samantha Power amesema baada ya kukutana na rais Salva Kiir kuwa baraza hilo limeweka wazi kwamba liko tayari kuweka vikwazo iwapo kutakuwa na watu wanaochafua mchakato wa amani , ama kuendelea na ukiukaji wa haki za binadamu.
Wawakilishi wa baraza hilo lenye wajumbe 15 , ambao wamewasili katika mji mkuu wa Juba jumatano wiki hii katika ziara ya siku mbili, wanatarajiwa kukutana na kiongozi wa waasi Riek Machar.
Maelfu ya watu wameuwawa na zaidi ya watu milioni 1.5 wamekimbia makaazi yao kutokana na mapigano yaliyochukua zaidi ya miezi minane yaliyozushwa na mvutano wa kutaka madaraka kati ya rais Salva Kiir na naibu wake aliyemfuta kazi Riek Machar.