NEC yatarajiwa kumtangaza mshindi wa uchaguzi wa urais leo
Tume ya taifa ya uchaguzi nchini Tanzania inatarajiwa kumaliza kutangaza matokeo ya urais hivi leo Alhamisi Oktoba 29.
Imechapishwa:
Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mstaafu Damian Lubuva Jumatano jioni wiki hii alitangaza kuwa tayari matokeo ya majimbo 195 yameshatangazwa na yanayosalia ni 69.
Jaji Lubuva ameongeza kuwa ikiwa tume itafanikiwa kumaliza kutangaza matokeo hayo hivi leo Alhamisi, mshindi atatangazwa na kupewa cheti.
Hadi Jumatau wiki hii mgombea wa chama cha Mapinduzi John Pombe Magufuli alikuwa anaongoza matokeo ambayo mgombea wa upinzani Edward Lowasa amesema hayatambui na ameitaka tume kusitisha kuyatangaza kwa tuhma za wizi wa kura.
Hayo yakijiri serikali ya Marekani inasema imestushwa na tamko la Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar hapo jana kufuta matokeo ya uchaguzi wa urais wa Zanzibar.
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi huko Zanzibar ZEC Jecha Salim Jecha jana alitangaza kufuta uchaguzi huo kwa kile alichokisema kuwa haukuwa huru na haki.