Rais wa Cameroon apunguza hukumu kwa wafungwa
Wafungwa wengi nchini Cameroon wameanza kuachiliwa kufuatia amri ya rais Paul Biya kupunguza adhabu yao. Mapema wiki hii Rais wa Cameroon Paul Biya ametangaza kuachiliwa huru kwa wafungwa ambao hakutaja idadi.
Imechapishwa:
Amri hiyo iliyoanza kutekelezwa Alhamisi wiki hii, japo haisemi ni mkakati wa kupambana na Corona, imepunguza kifungo cha wafungwa huku waliohukumiwa kifo wakihitajika kutumikia kifungo cha maisha.
Hatua hii inakuja katika muktadha uliowekwa katika siku za hivi karibuni baada ya baadhi ya mashirika ya kiraia na vyama vya siasa kutoa wito wa kuwaachilia huru wafungwa, ambao wanakabiliwa na hatari ya maambukizi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa hatari wa Covid-19.
Kutokana na amri hiyo, watu kati ya 2000 hadi 3000 wataachiliwa huru, kwa mujibu wa Maximilienne Ngo Mbe kutoka shirikisho la wanaharakati wa haki za binadamu katika ukanda wa Afrika ya Kati.