Ethiopia, Misri na Sudan kukutana tena kwa mazungumzo Jumanne
Mazungumzo mengine kati ya Ethiopia, Sudan na Misri, kujaribu kupata mwafaka kuhusu matumizi ya maji ya Mto Nile kufanikisha mradi mkubwa wa kuzalisha umeme, yameahirishwa hadi kesho.
Imechapishwa:
Afrika Kusini inaongoza mazungumzo haya, wakati huu Ethiopia ikiendelea kusisitiza kuwa, itaendelea na mradi huo, licha ya pingamizi kutoka kwa Misri inayosema tegemeo lake kubwa la maji ni Mto Nile.
Hivi karibuni serikali ya Misri ilitangaza kujiondoa kwenye mazungumzo na Ethiopia kuhusu mzozo wa ujenzi wa bwawa la Renaissance. Hii ni baada ya Ethiopia kuanza mchakato mpya wa kujaza bwawa hilo.
Ethiopia inasema kukamilika kwa mradi huo mkubwa barani Afrika, ni muhimu sana kwa mustakabili wa taifa hilo na utawaondoa mamilioni ya raia wake kutoka kwenye umasikini na kusambaza umeme barani Afrika.
Misri ilitaka kupewa maelezo na serikali ya Ethiopia kuhusu hatua hiyo, ikisema nchi hiyo itategemea asilimia 90 ya maji safi kutoka kwenye mto Nile na mradi huo unatishia uhai wa raia wake.
Mazungumzo ya kimataifa yakiongozwa na Marekani na Umoja wa Mataifa kujaribu kutatua mvutano huu, hayakufua dafu.