Mwaka mmoja umepita tangu rais John Magufuli aage dunia
Nchini Tanzania, ni mwaka mmoja tangu kufariki dunia kwa rais wa awamu ya tano John Magufuli, kifo kilichotokea ghafla na kuleta mshtuko ndani na nje ya nchi.
Imechapishwa:
Kifo cha Magufuli, kilitangazwa na Makamu wake wa rais wakati huo, Samia Suluhu Hassan, ambaye alieleza kuwa, Magufuli alifariki kwa matatizo ya moyo.
Kabla ya tangazo hilo, Magufuli hakuwa ameonekana kwa siku kadhaa na watu walianza kuzua uvumi kuhusu hali ya afya yake.
Siku mbili baadaye, Machi tarehe 19, Samia aliapishwa kuwa rais wa awamu ya sita, na kuwa mwanamke wa Kwanza kuongoza nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Baada ya kifo cha Magufuli, ambaye wapinzani wake walimshtumu kwa kuminya haki ya kujieleza na uhuru wa vyombo vya Habari, pamoja na kutoonekana kupambana ipasavyo na janga la Covid 19, ambalo lilisababisha maafa nchini humo, wakiwemo vigogo wa serikali akiwemo Makamu wa Kwanza wa Rais visiwani Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad.
Hata hivyo, alipoingia madarakani siku mbili baadaye rais Samia alivalia njuga suala la kupambana na janga hilo, na kuwahimiza Watanzania kuvalia barakoa na kupokea chanjo.
Aidha, amekumbatia wanawake kwenye serikali yake, baada ya kumteau Waziri wa Ulinzi mwanamke na kushawishi mwanamke kuchaguliwa kama spika wa bunge .
Samia pia ameonekana akizuru nje ya nchi yake na kuwahimiza wawekezaji kuja nchini mwake. Kuhusu siasa, ameonekana akitaka maridhiano baada ya kuachiwa huru kwa kiongozi Mkuu wa upinzani Freeman Mbowe na kukutana na Tundu Lissu jijini Brussels.