EU inashirikiana na DRC kuboresha ufuatiliaji wa rasilimali za taifa hilo
Umoja wa Ulaya umesema unafanya kazi na serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ambayo inaishutumu Rwanda kwa kupora madini yake, ili kuboresha ufuatiliaji wa rasilimali za taifa hilo, mjumbe wa umoja huo mjini Kinshasa amethibitisha.
Imechapishwa:
Cheza - 00:51
Kauli ya EU imekuja baada ya mwezi Februari Rais Felix Tshisekedi, akosoe mkataba uliotiwa saini kati ya umoja huo na Rwanda kuhusu usambazaji wa madini kwenye bara hilo, kitendo alichosema ni sawa na uchochezi.
Rwanda na DRC, kwa muda sasa zimekuwa katika vita ya maneno, Kinshasa ikiishutumu Kigali kwa kuunga mkono waasi wa M23 wanaoendelea kutatiza usalama mashariki mwa nchi hiyo, utawala wa Kigali hata hivyo ukikanusha madai ya Tshisekedi kwamba "inajificha" nyuma ya kundi hilo.
Hivi karibuni DRC imedai Rwanda imekuwa ikiiba madini kutoka kwenye migodi ya nchi hiyo na kwamba inauchukulia mkataba Wake na Brussels kama uhuni.
Balozi wa Umoja wa Ulaya Nicolas Berlanga Martinez, aliwaambia waandishi wa habari kuwa, umoja huo "unapaswa kueleza vizuri" undani wa makubaliano na Rwanda, na pia kufanyia kazi mtazamo wa DRC kuhusu hilo.
Juma moja lililopita, Kinshasa ilitishia kuishtaki kampuni ya Apple kwa kutumia malighafi za madini kutoka Kongo ambazo ilinunua kutoka kwa Serikali ya Rwanda, mawakili wakisema kitendo hicho ni sawa na kufadhili mauaji yanayoendelea mashariki mwa nchi hiyo.