Uganda: Waziri Engola auawa kwa kupigwa risasi na mlinzi wake
NAIROBI – Waziri wa kazi nchini Uganda Charles Engola, amepigwa risasi na kuuawa na mlinzi wake Jumanne hii, kwa kile kilichoelezwa ni kwa sababu ya mzozo wa malipo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 00:15
Tukio hilo lilitokea katika makaazi ya Waziri huyo, viungani mwa jiji la Kampala ambapo baada ya kutekeleza mauaji hayo, mlinzi huyo pia alijiua.
Walioshuhudia waliripoti kuwa mlinzi huyo alilalamika kuhusu hali yake ya maisha kabla ya kumpiga risasi waziri kisha kujiua baadaye
Hapa ni Luteni kanali Deo Akiiki Naibu msemaji wa jeshi la Uganda -UPDF
Tunapata mishahara yetu ifikapo tarehe 27 ya kila mwezi na kila askari alipata malipo yake kwa hivyo sidhani kama ni sababu ya yeye kufanya hivvyo, amesema Luteni kanali Akiiki
Baadhi ya watu wameelezea wasiwasi wao juu ya afya ya akili ya wanajeshi. Miongoni mwao ni Naibu spika wa bunge Thomas Tayebwa
Lazima tutafakari juu ya nini kingeweza kusababisha hii. Kwa upande wangu tuangalie afya ya akili ya watu hawa. Ni muhimu sana, amesema Tayebwa.
Meya wa Jiji la Kampala Erias Lukwago alitoa maoni yake kuhusu tukio hili, akisema huenda ni hasira iliyomfanya kutekeleza hili.
Hii ni hasira dhidi ya wale ambao wanaishi maisha ya ubadhirifu, hivyo hasira yake kwa maskini dhidi ya matajiri, amesema Lukwago.
Uchunguzi wa kisa hicho umeanza kwa mujibu wa msemaji wa polisi Fred Enanga.
Uchunguzi kwa sasa uko katika hatua za awali za uhakiki. Pia tulituma timu ya wataalamu wa matukio ya uhalifu ambao wanatumia teknolojia ya hali ya juu zaidi ya uchunguzi ili kupata ni nini hasa kilichosababisha mauaji haya ya kutisha.
Marehemu waziri Charles Engola ambaye hapo awali aliwahi kuwa naibu waziri wa ulinzi ni miongoni mwa viongozi wa Serikali waliotaka wafanyakazi wahudumiwe vizuri alipokuwa akizungumza katika kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani.
Kenneth Lukwago, Kampala, RFI Kiswahili