Ujenzi wa bomba la mafuta la Afrika Mashariki kuendelea: Mahakama
Nairobi – Mahakama ya kikanda imetupilia mbali rufa iliyokuwa inalenga kusitishwa kwa ujenzi wa mradi wenye utata wa Dolla Bilioni nne wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka nchini Uganda hadi taifa la Tanzania.
Imechapishwa:
Mahakama ya Afrika Mashariki kuhusu haki (EACJ) hapo jana Jumatano katika uamuzi wake, ilisema kuwa kesi hiyo ya kupinga mradi huo, iliwasilishwa kwa kuchelewa kwa hivyo ilikuwa imepitwa na muda na haikuwa na uwezo wa kuisikiliza.
Mradi huo wa kilomita 1,443 sawa na maili (896) wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), unaojengwa na serikali za Uganda na Tanzania kwa ushirikiano wa kampuni ya mafuta ya TotalEnergies kwa pamoja na kampuni ya mafuta ya China (CNOOC) umekuwa ukipingwa na jamii na watetezi wa mazingira.
Kwa mujibu wa makundi hayo ya kulinda mazingira, mradi huo unawaondoa raia ambao bomba hilo litapita katika maeneo yao kutoka kwa makazi yao.
Kando na kuwaondoa raia kwenye ardhi yao, watetezi wa mazingira aidha wanasema kuwa mradi huo unafukua makaburi ya wafu kwenye njia ya bomba hilo ambapo pia unachangia athari kwa mazingira.
Shirika la Natural Justice na mashirika mengine matatu ya kiraia ambayo yaliwasilisha kesi hiyo mahakamani mwaka wa 2020, yanasema yatakata rufa dhidi ya uamuzi huo.