DRC: Wagombea wa urais wameelekeza kampeni zao mashariki mwa nchi
Nchini DRC, wagombea mbalimbali katika uchaguzi wa mwezi huu wameelekeza kampeni zao katika eneo la mashariki linalokabiliwa na utovu wa usalama.
Imechapishwa:
Licha ya kuwa na utajiri wa madini, nchi hiyo ya Afrika ya kati imekuwa ikikabiliwa na utovu wa usalama, ufisadi pamoja na matumizi mabaya ya afisi za serikali.
Japokuwa sehemu kubwa ya taifa hilo imerejelea hali ya utulivu mdogo baada ya matukio mawili makubwa ya mapigano kati ya miaka ya 1990 na 2000, makundi ya watu wenye silaha na waasi, yamekuwa yakitekeleza mashambulio mashariki mwa taifa hilo jirani na nchi za Uganda, Rwanda na Burundi.
Kwa karibia miaka 30, miji ya Bukavu, Bunia, Butembo, Beni, Goma na Oicha imekuwa ikikabiliwa na machafuko.
Karibia raia milioni 44 kati ya idadi ya karibia watu milioni mia moja wamesajiliwa kushiriki katika uchaguzi huo mwa tarehe 20 ya mwezi huu wa Desemba.
Kando na uchaguzi wa urais, raia wa DRC pia wanawachagua viongozi wapya katika nyadhifa mbalimbali katika Wilaya na mitaa.
Mfanyibiashara tajiri kwenye taifa hilo na mwanasiasa wa upinzani Moise Katumbi, mmoja kati ya wagombea 23 wanaowania kiti cha urais, alikuwa wa kwanza kwenda mjini Goma, mji mkuu wa Kivu Kaskazini.
Baadhi ya raia katika mji huo wa Goma, wamesema wanatarajia wagombea hao wa urais kutatua suala la usalama.
Wagombea wa upinzani akiwemo Moise Katumbi, wamekuwa wakimtuhumu rais wa jamhuri ya kidemokrasia ya Congo anayemaliza muhula wake, Felix Tshisekedi kwa kushindwa kukabili changamoto za kiusalama haswa katika kulidhibiti kundi la waasi wa M23 amabo wamekuwa wakitekeleza mashambulio dhidi ya raia wa mashariki ya nchi hiyo.
Tshisekedi, ambaye anasaka kuongoza kwa muhula wa pili wa miaka mitano, naye pia anatarajiwa kutembelea eneo la mashariki ambapo atazuru mji wa Bunia,mkowani Ituri siku ya Jummane wiki ijayo.
Mkuu huyo wa nchi amewataka wapiga kura kumchagua tena ili kumpa nafasi ya kumaliza miradi mbalimbali aliyoaanzisha.
Machafuko huko Ituri, yamesababisha watu milioni 1.7 kutoroka vijiji vyao.
Naye mshindi wa Tuzo la Nobeli, Dkt Denis Mukwege, alizindua kampeni zake siku ya Jumapili ya wiki iliyopita katika mji wa Bukavu alikozaliwa katika jimbo la Kivu Kusini.
Martin Fayulu ambaye naye bado anazidi kudai kuwa aliibiwa kura katika uchaguzi wa urais wa mwaka wa 2018 pia anaendelea na kunadi sera zake, ambapo pia anatarajiwa kutembelea mji wa Beni huko Kivu kaskazini siku hiyo ya Jumanne.