Wakimbizi wa Sudan wathibitishwa kuambukizwa kipindupindu nchini Uganda
Nairobi – Raia 13 wa Sudan waliotoroka mapigano nchini mwao kati ya jeshi la serikali na wapiganaji wa RSF, wameripotiwa kulazwa nchini Uganda kutokana na maambukizo ya ugonjwa wa kipindupindu.
Imechapishwa:
Hatua hii imekuja baada ya kutokea kwa mlipuko wa ugonjwa huo katika wilaya ya Adjumani kaskazini mwa Uganda.
Kwa mujibu wa mamlaka ya afya kwenye eneo hilo, watu wanne kati ya 13 hao, wamethibitishwa kuambukizwa kipindupindu.
Mamlaka kwa sasa inapanga kuwatafuta karibia raia wengine 82 walioripotiwa kutangamana na watu hao walioambukizwa iliwafanyiwe vipimo.
Kipindupindu ni ugonjwa unaoambukiza kupitia maji na unasababisha mgonjwa kuharisha, kukosa maji mwilini na unaweza kuwa hatari kwa aliyeambukizwa katika kipindi cha muda mchache.
Mlipuko wa kipindupindu uliripotiwa kwa mara nyengine nchini Uganda mwezi Julai mwaka jana. Nchi ya Sudan nayo pia ikiripoti maambukizo hayo mwezi Septemba mwaka wa 2023.
Nchi za Zimbabwe, Msumbiji na Zambia nazo pia zinakabiliwa na msambao wa ugonjwa huo.