Watu 2 washtakiwa Kenya kwa mauaji ya mwanariadha wa mbio za masafa marefu kutoka Uganda
Wanaume wawili wameshtakiwa Jumatano nchini Kenya kwa mauaji ya mwanariadha wa mbio za masafa marefu wa Uganda Benjamin Kiplagat, ambaye alipatikana kwa kuchomwa kisu hadi kufa usiku wa kuamkia mwaka mpya.
Imechapishwa:
David Ekhai Lokere na Peter Ushuru Khalumi wamekanusha mashtaka walipofika mahakamani Eldoret, Bonde la Ufa. Ombi lao la kuachiliwa kwa dhamana lilikataliwa kutokana na rekodi yao ya uhalifu na hatari ya wao kutoroka. Lokere, 25, na Khalumi, 30, walikamatwa Januari 1, saa chache baada ya kupatikana kwa mwili wa mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 34, aliyechomwa kisu shingoni.
Polisi wa Kenya iliwataja wanaume hao wawili "wahalifu wanaojulikana ambao waliwatishia watu" karibu na Eldoret, ambapo mwili wa Kiplagat ulipatikana kwenye gari. Ingawa chanzo cha mauaji hayo bado hakijajulikana, polisi ilisema mwathiriwa aliyekuwa akisafiri kwa gari "alishambuliwa" na watu hao wawili waliokuwa kwenye pikipiki.
Mji wa Eldoret katika Bonde la Ufa huwaona wanariadha wengi waliobobea katika mbio ndefu na za kati kuja kufanya mazoezi ili kunufaika na mwinuko.
Kiplagat, mzaliwa wa Kenya na mwenye umri wa miaka 34, alikuwa amewakilisha Uganda katika mbio za mita 3,000 kuruka viunzi katika matoleo kadhaa ya Michezo ya Olimpiki na michuano ya dunia. Kifo chake kilifuatia mauaji ya Oktoba 2021 ya nyota wa mbio za masafa marefu Mkenya Agnes Tirop, 25, ambaye alipatikana akiwa nyumbani kwake huko Iten, kituo cha mafunzo cha mwinuko karibu na Eldoret.
Familia ya Kiplagat inabaini kwamba hakulengwa kibinafsi bali alikuwa mwathiriwa wa wezi. Benjamin Kiplagat, aliyezikwa nchini Kenya, ameacha mke mjamzito, Viola, na binti wa miaka 13.