Rwanda yalituhumu shirika la HRW kuwa kipaza sauti cha makundi ya kigaidi
Serikali ya Rwanda imelituhumu shirika la kimataifa la kutetea haki za bunadamu dunuani la Human Right Watch, kuwa ni shirika linalopaza sauti na kutetea maslahi ya makundi ya kigaidi duniani.Kwenye taarifa iliyotolewa hivi leo kwa vyombo vya habari vya Rwanda na wizara ya sheria nchini humo, imesema kuwa shirika la Human Right Watch limekuwa likisaidia makundi ya kigaidi kueneza propaganda zao duniani.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwenye taarifa hiyo iliyochapishwa kwa kirefu kwenye gazeti la Serikali la New Times, imesema kuwa kwa kipindi kirefu sasa shirika hilo limekuwa mstari wa mbele kueneza propaganda za makundi ya kigaidi na hasa wanasiasa ambao hawaitakii mema nchi ya Rwanda.
Wizara hiyo inasema kuwa "Kwa nchi ya Rwanda imekuwa ni jambo linalokanganya sana kwasababu tunashindwa kuelewa majukumu ya shirika hili na majukumu ya makundi ya kigaidi". Imesema taarifa hiyo ya wizara iliyoitwa tathmini ya mashirika ya kiraia.
Wizara ya sheria nchini humo imetishia kupitia upya sheria inayoruhusu taasisi hizo kufanya kazi nchini Rwanda na kwamba itaongeza kipengele ambacho kitayataka mashirika yote nchini humo kueleza shughuli mahsusi ambazo inazifanya.
Wizara hii imeongeza kuwa kutokana na makubaliano ya awali kuonekana kukiukwa, inaifanya sasa Serikali kupitia upya makubaliano ya shirika hilo kuwepo nchini Rwanda kwa kile ilichodai shirika hilo limevuka mipaka na kusababisha hasara ambayo kwasasa haiwezi kufidiwa.
Taarifa ya wizara ya Sheria nchini Rwanda imeongeza kuwa kwasasa shughuli za shirika hilo unaweza ukazitafsiri kwa sentensi moja tu, ya kwamba limekuwa ni shirika linaloendesha propaganda mbaya kwa nchi ya Rwanda.
Wizara hiyo imelitaja shirika hili lenye makao yake makuu nchini Marekani, ya kwamba limekuwa ni shirika ambalo ni kipasa sauti kwa makundi ya kigaidi na hasa kundi la waasi wa kihutu wenye asili ya Rwanda FDLR la nchini DRC, kundi ambalo utawala wa raus Paul Kagame umelitaja kama kundi la kigaidi.
Kundi la FDRL lenye wapiganaji wa kihutu linashutumiwa na utawala wa Rwanda pamoja na Umoja wa Mataifa kwa kuhusika na mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 ambapo zaidi ya watutsi laki nane waliuawa.
Hivi karibuni shirika la Human Right Watch limejikuta kwenye mzozo na Serikali ya Rwanda baada ya kutoa taarifa inayoitaja nchi hiyo kufadhili makundi ya waasi wenye silaha wanaopigana mashariki mwa DRC.