Sudani Kusini : Riek Machar akataa kuwa makamu wa pili wa rais
Kiongozi wa waasi Sudan Kusini Riek Machar, amebaini kwamba kamwe hawezi kuchukua mamlaka aliyopewa na rais Salva Kiir ya kuwa makamu wa pili wa rais katika taifa changa linalokumbwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. Ni taarifa ya mwandishi wa RFI Sudani Kusini, James Shimanyula.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 02:51
Riek Machar amesema kwamba hatokubali kujiunga na serikali dhaifu, hadi pale amani ya kudumu itapatikana.
“Nataka mapatano mwafaka ya kurejesha amani. Ni hayo mapatano halali na halisi ambayo yatatuongoza kuanzisha serikali ya mpito. Bila mapatano hayo na mwafaka wa kuleta amani ya kudumu, mimi siwezi kujiunga na serikali yoyote”, amesema Machar.
Akizungumza kuhusu kuhusu kauli hiyo ya Riek Machar kuchukua mamlaka hayo, waziri wa ulinzi wa Sudan Kusini Kuol Mnyang Juuk alishangazwa na sisitizo la Machar kuwa lazima rais Kiir ang’atuke mamlakani kabla ya mabadiliko mapya ya kisiasa kufanyika humo nchini.
“Riek Machar alipewa mamlaka ya makamu wa pili wa rais, lakini amekataa kutwaa mamlaka hayo. Anataka Rais Salva Kiir ang’atuke madarakani. Hiyo ndiyo sababu inayomfanya akatae kuwa makamu wa pili wa rais”, amesema Juuk.
Juuk amebaini kwamba Riek Machar kamwe hawezi kutimiza ndoto yake ya utawala, iwapo amekataa wadhifa huo nakudhani kwamba siku moja atakua rais.
Makamu wa kwanza wa rais wa Sudan Kusini ni James Wani Igga, ambaye zamani alikuwa spika wa bunge la nchi hiyo.
Hayo yakijiri Usalama wa taifa nchini Sudan Kusini kwa mara nyingine umekifungia kituo pekee cha Radio kilichokuwa kinajitegemea na kuwakamata waandishi wake wakiwemo wahariri kwa madai ya kurusha habari zilizowahusu waasi wa Riek Machar.
Kituo cha Bakhita kinachomilikiwa na kanisa katoliki kama sehemu ya redio ya jamii, kilivamiwa na maofisa usalama mwishoni mwa juma, na kutangazwa kufungwa baada ya kutangaza habari zinazohusu waasi ikiwa ni pamoja na kuanza upya kwa mapigano kati ya vikosi vya serikali na waasi hao.
Tayari mkurugenzi wa kituo hicho ameandika barua kwa serikali kuomba radhi kutokana na kuripoti habari na maoni yaliyotolewa na waasi kuhusu kuendelea kwa vita nchini humo.
Mwanzoni mwa mwezi huu mashirika ya kutetea haki za binadamu yalionya kuhusu operesheni zinazoendelea kufanywa na serikali ya Juba ya kuwakamata, kuwaweka kizuizini pamoja na kuzuia mijadala inayohusu namna ya kutatua mzozo ulipo kwasasa nchini humo.