Somalia: serikali yamtimua mkuu wa Intelijensia
Serikali ya somalia imechukua uamuzi wa kumtimua kiongozi mkuu wa intelijensia nchini humo kwa kile inachodai ameshindwa kutimiza wajibu wake.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Abdulahi Mohamed Ali, aliteuliwa mwezi julai mwaka huu ili kuimarisha juhudi za idara za usalama baada ya shambulizi la wanamgambo wa Al Shabab kutekelezwa katika ikulu ya raisi mjini Mogadishu.
Msemaji wa serikali Ridwan Haji Abdiweli ameeleza hii leo kuwa maamuzi hayo yamefikiwa baada ya baraza la mawaziri kufanya kikao cha dharura asubuhi ya jumatatu wiki hii kujadili masuala mbalimbali ikiwemo usalama na kubaini kiongozi huyo kushindwa kutimiza wajibu aliopatiwa.
Msemaji huyo wa serikali hakufafanua zaidi kuhusu uamuzi huo ingawa wanamgambo wa al shabab wameendelea kufanya mashambulizi makali mjini mogadishu ikiwemo dhidi ya makao ya bunge na makao makuu ya ofisi za usalama wa taifa.
Hayo yakijiri waandishi wa habari wanne wa redio za kibinafsi za Mogadiscio, wametiwa nguvuni na wakuu wa Somalia kwa kutangaza habari za wapiganaji wa Al Shabab.
Kushikwa kwao kunakuja muda mfupi baada ya serikali ya Somalia kupiga marufuku kurushwa hewani habari ama kuchapisha magazetini habari kuhusu wapiganaji wa Al Shabab.
Kati ya waandishi hao wanne kuna Osman Abdulilahi Guled, mhariri mkuu wa redio ya kibinafsi ya Kumle.
Majina ya waandishi wengine waliotiwa nguvuni hayakutolewa na wakuu hao lakini inasadikika kuwa walikuwa wahariri katika vituo vya kibinafsi vya radio Shabelle na Sky FM.
Serikali ya Somalia inadai kuwa waandishi hao wamekuwa wakirusha habari za Al Shabab na kuzipa kipaumbele kuliko habari nyingine hasa zinazohusu ushindi wa vikosi vya serikali na vya AMISOM ambavyo vinatoka Uganda, Djibouti, Kenya, Sierra Leone, Ethiopia na Burundi.
Mohamed Ibrahim, katibu mkuu wa chama cha waandishi nchini Somalia, akiongea na idhaa ya Kiswahili ya RFI amekemea tabia hiyo ya serikali ya kuwatia nguvuni waandishi wakati wametekeleza kazi yao ya kutafuta habari kuichunguza na kuirusha hewani aidha kuichapisha.
“Serikali haitaki radio za kibinafsi zitangaze habari za Al Shabab. Hii ina maana kuwa kamwe waandishi hawaruhusiwi kuwahoji Al Shabab. Hii pia ina maana kuwa habari zote zinazohusu Al Shabab zimepigwa marufuku”, amesema Ibrahim, huku akibaini kwamba serikali ya Somalia haitaki kusikia msemaji yeyote wa Al Shabab akinukuliwa kwenye redio zinazorusha matangazo yake hapa Somalia.