Kundi la Al Shabab lamtangaza kiongozi mpya baada ya kuuawa kwa Godane
Kundi la wanamgambo wa Al Shabab limetangaza kumchagua kiongozi mpya wa kundi hilo kufuatia kuuawa kwa kiongozi wao Ahmed Abdi Godane katika shambulizi la anga lililotekelezwa na wanajeshi wa Marekani mjini Mogadishu siku ya Jumatatu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Pia kundi hilo limeapa kulipiza kisasi kwa kifo cha kiongozi wao na kusema kwamba litaendeleza mashambulizi yao kuiangusha serikali ya Somalia inayoungwa mkono na mataifa mbalimbali duniani.
Taarifa ya kundi hilo iliyochapishwa kwenye mtandao wa jihadi na kuthibitishwa na maafisa wa kundi hilo imetolewa baada ya serikali ya Somalia kuonya kuhusu uwezekano wa mashambulizi ya kisasi kutoka kwa kundi hilo.
Serikali ya Somalia imeonya kuwa huenda nchi hiyo ikakumbwa na wimbi la mashambulizi ya kisasi ya wanamgambo wa Al Shabab baada ya kiongozi wao kuthibitishwa kuuawa kwenye shambulizi la anga lililotekelezwa na Marekani.
Rais wa nchi hiyo ya pembe ya Afrika pia amewapa nafasi wanamgambo wa Al Shabab kuweka silaha zao chini na kuachia maeneo wanayoshikilia kwa msamaha wa siku 45, akiwaambia kwamba vikosi vya serikali na vya Umoja wa Afrika AMISOM wakombioni kuvamia maeneo yao.
Siku ya Ijumaa Marekani imethibitisha kuuawa kwa kiongozi wa wanamgambo hao wa al-Shabab, Ahmed Abdi Godance, katika shambulizi lililotekelezwa na wanajeshi wake mapema siku ya Jumatatu.