Watanzania wabaki njia panda kuhusu hatima ya upotevu wa mabilioni ya fedha,baada ya mjadala kuahirishwa
Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeshindwa kamilisha hatua ya kujadili na kupitisha maazimio kutokana na kamati ya bunge ya hesabu za serikali, PAC kuhusu ripoti ya kashfa ya IPTL na akaunti ya ESCROW TEGETA baada ya kutokea mvutano mkali miongoni mwa wabunge.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kutokana na mvutano huo ulioibuka wakati wa kufanya maamuzi juu ya mapendekekezo ya kamati hiyo ya PAC Spika wa bunge Anne Makina alilazimika kuahirisha kikao cha Bunge hadi watakaposhauriana tena.
Kauli hiyo ya Spika Makinda ililazimika kutolewa baada ya wabunge wa upande kambi ya upinzani wengi wao kusimama wakipinga kuburuzwa katika hatua ya kufanya maamuzi ndipo kiongozi wa kambi rasmi ya Upinzani Freeman Mbowe akakosoa mchakato huo.
Hoja iliyoibua mjadala mzito ni ile ya kutaka kuwajibishwa kwa viongozi wa serikali akiwemo katibu mkuu wa wizara ya nishati na madini, naibu na waziri wake pamoja na mwanasheria mkuu wa serikali hatua ambayo ilipingwa na wabunge wa Ccm.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wanaona kuwa Bunge hilo limeshindwa kutimiza wajibu wake baada ya kushindwa kuafikiana.
Bunge hilo lilijadili ripoti ya Kamati ya Bunge ya hesabu za serikali yenye dhamana ya kuchunguza kashfa hiyo ya IPTL ikiongozwa na mwenyekiti Zitto Kabwe ambayo kwa kiasi kikubwa ilishinikiza kuwajibika kwa viongozi waliotajwa kuchota fedha na kutotimiza wajibu wao.