Gilbert Diendéré na Djibrill Bassolé wakabiliwa na mashtaka
Jenerali Gilbert Diendéré na Djibril Bassole Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje wa aliyekuwa rais wa Burkina Fasso Blaise Compaoré wanakabiliwa na mashtaka kumi na moja kwa kuhatarisha usalama wa taifa mwezi uliopita.
Imechapishwa:
Wawili hao wanaotuhumiwa kwa jaribio la mapinduzi ya tarehe 17 mwezi uliopita nchini humo walifikishwa mahakamani jana kujibu mashtaka kwa kuhusika katika mapinduzi yaliyopangwa na Kikosi cha ulinzi wa rais.
Jenerali Gilbert Diendéré ambaye ni Kiongozi wa Kikosi hicho nchini Burkina Faso alikamatwa siku chache zilizopita pamoja na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa rais Blaise Compaoré Djibril Bassole na kuhojiwa na jaji mmoja kama sehemu ya uchunguzi kwa kushtakiwa kwa kuhatarisha usalama wa taifa.
Watuhumiwa hao pia wanashitakiwa kwa kula njama na vikosi vya kigeni kudhoofisha usalama wa ndani na kulenga kuiondoa madarakani Serikali ya mpito ikiwa ni pamoja na makundi ya kijihadi kwa utekelezaji wa mapinduzi hayo yaliyofanywa na askari wa zamani wa ulinzi wa rais.
Jenerali Diendéré na Bassole pia wanashitakiwa kwa mauaji, na kujeruhi watu kwa kukusudia, kula njama za kushambulia na uharibifu wa makusudi wa mali za umma ambapo baada ya kusomewa mashitaka yote kumi na moja wameendelea kuwekwa chini ya ulinzi hadi watakapohojiwa tena.