Sudani: Mali za ndugu na washirika wa Omar al-Bashir zakamatwa
Mahakama nchini Sudani inaendelea kuangamiza mfumo wa serikali ya zamani nchini humo. Mali za ndugu na washirika kadhaa wa dikteta wa zamani wa Sudani Omar al-Bashir zimekamatwa.
Imechapishwa:
Tangazo hilo lilitolewa Alhamisi jioni na Kamati Maalum iliyoundwa mwezi Desemba mwaka jana ili kuvunja mtandao wa ufisadi wa utawala wa zamani, ambao ulianguka mwaka mmoja uliopita.
"Ukubwa wa ufisadi wakati wa utawala wa Omar al-Bashir unazidi kile mtu angeweza kufikiria," amesema Wadji Saleh, mmoja kati ya wajumbe wa kamati yenye jukumu la kukusanya mali zilizoporwa na serikali ya zamani.
Mali hizo zilizokamatwa ni nyingi, ikiwa ni pamoja na nyumba za kifahari, na pia karibu mita mraba 100,000 za ardhi. Mali zote hizo zimekuwa zinamilikiwa ndugu na washirika 20 wa dikteta wa zamani wa Sudani Omar al-Bashir, ikiwa ni pamoja na shemeji zake, wipwa zake au hata baadhi ya mawaziri wa zamani.
Bidhaa zilizopatikana kwa ubadhirifu wa mali ya umma au wizi kupitia uhusiano wa karibu na rais wa zamani, zitakabidhiwa Wizara ya Fedha.
"Enzi ambapo maafisa walichukua pesa kutoka kwa wanyonge imepitwa na wakati. Huu ni ujumbe kwa maafisa wa zamani na wa sasa, " ameahidi naibu mwenyekiti wa Kamati hiyo, Muhammad Al Faki Suleiman.