Uchaguzi Equatorial Guinea: Teodoro Obiang Nguema ashinda uchaguzi kwa muhula wa sita
Rais wa Equatorial Guinea Teodoro Obiang Nguema Mbasogo, ambaye tayari ametumia miaka 43 madarakani, ameshinda uchaguzi wa urais wa Novemba 20 kwa zaidi ya 94% ya kura.
Imechapishwa:
Kulingana na matokeo yaliyosomwa kwenye televisheni ya umma na Faustino Ndong Esono Eyang, Waziri wa Mambo ya Ndani ambaye pia ni mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, waliojitokeza kwa kupiga kura walikuwa 98%.
Rais Obiang Nguema, mgombea kwa muhula wa sita mfululizo, alipata 94.9% ya kura kati ya zaidi ya wapiga kura 413,000. Mpinzani wake mkuu, Andrès Esono Ondo, alipata kura 9,684 pekee, sawa na takriban 4% ya kura.
Upinzani bila ya kuwa na kiti bungeni
Kuhusu uchaguzi wa wabunge, Chama cha Kidemokrasia cha Equatorial Guinea (PDGE) cha Rais Obiang Nguema na vyama washirika 14 vimeshinda viti vyote 100 katika Bunge la kitaifa.
Ushind kama huo pia umeripotiwa katika Bunge la Seneti ambapo viti 55 pia viko chini ya udhibiti wa mamlaka. Lakini kwa vile Bunge hili linapaswa kuwa na wajumbe 70, hao wengine 15 watateuliwa na Rais wa Jamhuri kwa mujibu wa Katiba.